Monday, August 1, 2016

Maana ya fasihi simulizi na tanzu zake kwa mujibu wa wataalam mbalimbali


Maana ya fasihi simulizi
Fasihi simulizi ni sanaa ya matumizi ya lugha ya kubuni inayosambazwa kwa mdomo kwa njia ya kuimbwa, kughaniwa, kuigizwa, kusimuliwa, kuumbwa, kufumba au kutegeana mafumbo na vitendawili (Syambo na Mazrui, 1992:2) katika King’ei na Kisozi, (2005:7).
Mulokozi, (1996:24) anaeleza kuwa fasihi simulizi ni fasihi iliyotungwa au kubuniwa kichwani na kuwasilishwa kwa hadhira kwa njia ya mdomo na vitendo bila kutumia maandishi. Ni tukio linalofungamana na muktadha (mazingira) fulani wa kijamii au wa kutawaliwa na mwingiliano wa mambo kadhaa wa kadhaa kama vile, fanani, hadhira, fani, na maudhui yaliyokisudiwa na mwasilishaji.
TUKI, (2004) fasihi simulizi ni kazi ya fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo kama vile, hadithi, ngoma na vitendawili. Aidha, fasihi simulizi ni ile ambayo inapitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kupitia neno la mdomo (Ngure, 2003:1).
Kwa ujumla, tunaweza kusema kuwa fasihi simulizi ni fasihi inayotungwa na kuwasilishwa kwa hadhira kwa njia ya mdomo ambapo kuna uambatanishaji wa utendaji katika uwasilishaji huo. Fanani na hadhira huonana ana kwa ana jambo ambalo huwafanya hadhira kushiriki katika baadhi ya utendaji. Kwa mfano, kuimba, kucheza, au kupiga makofi na vigelegele.
Tanzu za fasihi simulizi
Wamitila, (2003) anadai kuwa tanzu ni istilahi inayotumika kuelezea au kurejelea aina za kazi mbalimbali za kifasihi.
Hivyo basi, kutokana na maana ya tanzu iliyotolewa na Wamitila, (2003) tunaweza kusema kuwa tanzu ni istilahi ya kifasihi inayotumika kumaanisha matawi au mafungu katika kazi za fasihi. Tanzu za fasihi simulizi zimeainishwa kwa namna tofauti tofauti kwa mujibu wa wataalamu mbalimbali kama ifuatavvyo:


Wamitila, (2008) katika uainishaji wake wa fasihi simulizi anazigawa tanzu za fasihi simulizi katika makundi yafuatayo:
Simulizi au hadithi; huu ni utngo wenye visa vya kubuni au halisi unaowasilishwa kwa lugha ya nathari kwa kusudi la kuburudisha, kukuza maadili na kuunganisha jamii. Katika usimuliaji wa hadithi fanani huwa mfaraguzi ili asiwachoshe watazamaji wake kwa kuingiza utendaji unaowashirikisha watazamaji wake.
Maigizo; ni sanaa inayotumia utendaji kuiga tabia au matendo ya watu wengine au viumbe wengine ili kuburudisha au kutoa ujumbe kwa jamii. Maigizo ni sanaa inayopatikana katika makabila mengi ya kiafrika na huambatana na utambaji wa ngoma. Kwa mfano, jando na unyago, malumabno ya watani na vichekesho.
Ushairi (nyimbo); ni sanaa ya uimbaji inayoambatana na mdundo wa ngoma au mziki ili kufikisha ujumbe kwa hadhira. Katika fasihi simulizi nyimbo huambatana na mdundo wa ngoma na mara nyingi nyimbo hizi huwa na mkutdha kulingana na ujumbe uliolengwa. Hivyo basi, tunapata nyimbo za ndoa/arusi, jando/tohara, hodiya, kimai, nyimbo za mazishi, nyimbo za kidini, nyimbo za kizalendo na nyimbo na mapenzi.
Semi; ni mafungu ya maneno ambayo hutumiwa kuleta maana nyingine badala ya maneno halisi ya maneno yaliyotumika. Katika fasihi ya Kiswahili semi hujumuisha nahau, misemo na methali. Kwa mfano, tukisema mtu amegonga mwamba hatumanishi kwamba amepiga jiwe kubwa kwa mkono au kwa kifaa chochote, bali tunamanisha kwamba ameshindwa kuendelea katika jambo fulani.





Mazrui & Syambo, (1992) wanasema kuwa fasihi simulizi ina tanzu zake ambazo ni tofauti na zile za fasihi andishi ingawa kuna baadhi amabazo zinafanana na zile za fasihi andishi. Fasihi simulizi ina tanzu kuu nne ambazo tunaziainisha kama ifuatavyo:
Ngano au hadithi; ni tungo yoyote ya kubuni inayosimuliwa kwa lugha ya nathari. Katika fasihi ya Kiswahili ngano ni za aina nyingi lakini zote huanza kwa njia inayofuata mtindo huu:
Msimulizi : Paukwa!
Msikilizaji : Pakawa!
Msimulizi : hapo zamani za kale palitokea…
Nyimbo au mashairi; kuna nyimbo za aina nyingi katika fasihi ya Kiswahili lakini zinazokusudiwa hapa ni zile zilizotungwa kwa mdomo (bila maandishi) na kusambazwa kwa mdomo. Nyimbo za aina hii zimeenea katika maisha ya Kiswahili na huwafata tangu wanapozaliwa mpaka kufa kwao. Nyimbo hizi kwa kawaida huwa zinafungamana na ngoma au michezo fulani na mara nyingine huimbwa pamoja na mziki kwa mfano, nyimbo za sherehe, nyimbo za watoto, nyimbo za taarabu na bembezi.
Methali; hii ni misemo mifupi yenye hekima fulani ndani yake. Methali hudhihirisha mkusanyiko wa mafunzo waliopata watu wa vizazi vingi vya jumuia fulani katika maisha yao. Methali hutumiwa sana katika mazungumzo ya kawaida ya waswahili na ni sehemu moja muhimu katika fasihi simulizi ya Kiswahili. Methali nyingi za Kiswahili huwa na mdundo maalumu wa kishairi na mara nyingine huwa na vina.
Vitendawili; ni tungo fupi ambazo huwa na swali fupi lisili wasi na jibu kwa makusudi ya kupima ufahamu wa hadhira kuhusu mazingira yake. Anayetoa kitendawili huuliza swali lake kwa kutoa maelezo mafupi yanayorejelea umbo la kitu hicho, sauti harufu au kukifananisha na kitu kingine. Anayejibu huhitaji kufkiria haraka na kutoa jawabu ambalo huwa na neno moja au maneno mawili hivi. Vitendawili huwa na mianzo maalumu kulingana na jamii yake. Katika fasihi simulizi vitendawili huwalenga watoto ili kuchochea fikra na kuwazoeaza mazingira yanayowazunguka.
Mulokozi katika makala yake ya tanzu za fasihi simulizi iliyo katika jarida la Mulika Na 21 (1989) amezigawa tanzu na vipera vya fasihi simulizi kwa kutumia vigezo viwili ambavyo ni:
  1. Umbile na tabia ya kazi inayohusika; katika kigezo hiki, Mulokozi ameangalia vipengele vya ndani vinavyounda sanaa hiyo na kuipa mwelekeo au mwenendo. Baadhi ya vipengele hivyo vya ndani ni namna lugha inavyotumika kishairi, kinathari, kimafumbo, kiwingo au kughani, muundo wa fani hiyo na wahusika.
  2. Muktadha; ambapo amezingatia kuwa fasihi simulizi ni tukio, hivyo huambatana na mwingiliano wa mambo matatu ambayo ni muktadha, watu na mahali. Mwingiliano huu ndio unaotupa muktadha na muktadha ndio unaoamua fani fulani ya fasihi simulizi ichukue umbo lipi, iwasilishwe vipi kwa hadhira kwenye wakati na mahali hapo. Hivyo hadithi inaweza kugeuzwa wimbo, utendi unaweza kuwa hadithi na wimbo unaweza kugeuzwa ghani au usemi kutegemea muktadha unaohusika. Kwa hiyo, Mulokozi amezigawa tanzu na vipera vya fasihi simulizi kama ifuatavyo:
Masimulizi; hii ni tanzu ya fasihi simulizi yenye kusimulia habari fulani. Katika kugawa utanzu huu vigezo vilivyotumika ni pamoja na kigezo cha lugha ambapo lugha iliyotumika katika masimulizi ni ya kinathari. Pia kigezo cha muundo kimetumika mara nyingi masimulizi huwa na muundo unaojitofautisha na tanzu nyingine kama vile ushairi. Mara nyingi katika masimulizi muundo wake huwa ni wa moja kwa moja yaani mtiririko wa visa na matukio. Vile vile kigezo kingine ni cha wahusika ambapo katika kigezo hiki huhusishwa wahusika wa pande mbili ambao ni mtendaji na watendwaji. Kigezo kingine ni kigezo cha namna ya uwasilishwaji. Katika uwasilishwaji, huwasilishwa na msimuliaji mbele ya hadhira. Kigezo kingine ni mandhari ambayo huwa ni maalumu kama vile chini ya mti mkubwa na uwanjani. Masimulizi pia hufanyika katika muda maalumu, kwa mfano baada ya kazi. Masimulizi yamegawnyika katika tanzu mbili ambazo ni tanzu za kihadithi (za kubuni) na tanzu za kisa huwa (kihistoria).
Utanzu wa semi; semi ni tungo au kauli fupi fupi za kisanaa zenye kubeba maana au mafunzo. Kigezo kilichotumika ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya mkato na kigezo kingine ni cha kidhima ambacho hufunza. Utanzu huu umegawanyika katika vipera vifuatavyo: methali, vitendawili, misimu, mafumbo na lakabu.
Ushairi; huu ni utanzu wa fasihi simulizi unaowasilishwa kwa hadhira kwa njia ya uimbaji au ughani badala ya usemaji wa kawaida. Vigezo vinavyotumika katika utanzu huu ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya kishairi. Pia kimetumika kigezo cha fani ambapo fani inayotumika ni wizani, lugha ya mkato, lugha ya mafumbo na uimbaji wa ughani. Vipera vya utanzu huu ni nyimbo na maghani.
Utanzu wa mazungumzo; mazungumzo ni maongezi au maelezo ya mdomo katika lugha ya kawaida juu ya jambo lolote lile. Si kila mazungumzo ni fasihi, ili mazungumzo yaitwe fasihi lazima yawe na usanii fulani. Vigezo vinavyotumika katika kugawa utanzu huu ni kigezo cha lugha ambapo lugha inayotumika ni lugha ya kifasihi. Kigezo kingine ni kigezo cha kimuundo ambapo muundo wake huwa wa kidayolojia. Vipera vya utanzu huu ni hotuba, soga, mawaidha, malumbano ya watani na ulumbi.
Maigizo; ni michezo ambayo hutumia watendaji wa kuiga tabia na matendo ya watu au viumbe wengine ili kuburudisha na hutoa ujumbe fulani kwa hadhira. Vigezo vilivyotumika katika kutenga utanzu huu ni kigezo cha namna ya uwasilishaji ambapo huwasilishwa kwa kuiga matendo ya watu na wanyama. Kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuburudisha, kuelimisha au kuonya. Pia kinatumika kigezo cha mandhari ambapo maigizo huambatana na matukio maalumu kama vile kwenye maadhimisho ya sherehe fulani na katika matukio ya kijamii.
Ngomezi; ni ile hali ya kupeleka ujumbe kwa kutumia mdundo wa ngoma. Vigezo vinavyotumika katika utanzu huu ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kupeleka taarifa fulani kwa jamii. Kwa mfano, taarifa hiyo yaweza kuwa ya msiba, mkutano na kadhalika.
Vile vile Okpewho, (1992) amazigawa tanzu za fasihi simulizi kwa kuzingatia vigezo vinne kama ifuatavyo:
  1. Kigezo cha unguli; katika kigezo hiki kuna jitokeza ngano zosozohusu wanadamu. Kuna ngano za wanyama, ngano za vichimbakazi na ngano za miungo. Hata hivyo kigezo hiki kinaonekana kuwa na matatizo kadha wa kadha kama vile kufanana kitabia kati ya jamii moja na nyingine, kupuuza namna mbalimbali katika ngano ambazo vichimbakazi, wanadamu na wanyama huhusiana.
  2. Kigezo cha lengo la ngano husika; katika kigezo hiki ngano zinaainishwa kwa kuzingatia lengo la simulizi husika. Hapa panajitokeza ngano za kimaadili, ngano za kuhimiza kazi na zinginenzo.
  3. Kigezo cha sifa ya ubora wa ngano; ni kigezo ambacho ndicho kinaonekana kubeba kundi kubwa la ngano. Katika kigezo hiki kuna ngano ayari (ambazo huambatana na uelevu au ulaghai wa wahusika) ngano za mtanziko kama vile zinazohusu vita , vizazi, mashujaa na zinginezo.
  4. Kigezo cha muktadha au utendaji wa ngano husika; katika kigezo hiki kinachoangaliwa ni ngano inatendwa wakati gani na katika mazingira gani. Kwa mfano, kwa kutumia kigezo hiki tunaweza kupata ngano za mbalamwezi, ngano za ibada, ngano zinazotendwa wakati wa mapumziko ya wawindaji na zinginezo.
Hivyo basi, Okpewho, (1992) amezigawa tanzu za fasihi simulizi katika makundi yafuatayo:
Nyimbo na maghani; ni sanaa ya kuwasilisha ujumbe kwa hadhira inayoambatana na mdundo wa ngoma au mziki. Katika uimbaji fanani hutoa sauti inayoendana na mapigo ya ngoma au mziki. Aghalabu nyimbo hizi huweza kuimbwa katika tukio maalumu. Hivyo basi, tunaweza kuainisha nyimbo katika makundi mablimbali kama vile bembezi, mbolezi, sifo na zinginezo.
Masimulizi; ni visa vya kubuni au halisi vinavyowasilishwa kwa hadhira kwa kutukia lugha ya nathari. Katika masimulizi fanani huwasilisha ujumbe wake kwa njia ya kuisimulia hadhira yake kwa kutumia mbinu mbalimbali zinazoambatana na utendaji.
Semi; ni tungo fupi fupi zenye hekima na busara ndani yake. Mara nyingi kinachozungumzwa ni tofauti na kilichokusudiwa. Wakati mwingine tungo hizi hutumika ili kuipa adabu lugha ya mzungumzaji. Kwa mfano, Juma ana mkono wa birika katika tungo hii tukifasili kuwa juma anamkono unaofanana na wa birika tunapoteza maana ya tungo hiyo.
Ngonjera; ni nyimbo ambazo huhusisha waimbaji zaidi ya mmoja, uimbaji wao huwa katika mfumo wa majibizano. Aidha utanzu huu huweza kuitwa kuwa ni ushairi wa maigizo maan huwa kuna jambo ambalo waimbaji hawa hulumbana ingawa mwishoni hufika hitimisho kwa mmjo wao kukubaliana na mawazo yaw engine.
Aidha, Balisidya, (1987) anaigawa fasihi simulizi katika tanzu tatu kama ifuatavyo:
Nathari; katika nathari anatoa vipera kama vile ngano-istiara, harafa na hekaya, tarihi-kumbukumbu, shajara, hadithi za kihistoria pamoja na epiki, visaasili- kumbukumbu na tenzi.
Ushairi; katika ushairi kuna vipera kama vile nyimbo-tahlili, bembea, tumbuizo, ngoma, miviga, watoto na kwaya, maghani, majigambo, vijighani, shajara, pamoja na tenzi.
Semi; katika utanzu huu kuna vipera kama vitendawili, misimu, mafumbo, methali-msemo na nahau, misimu-utani, masaguo na soga.
Tukiwaangalia wataalamu hawa wanatofautina katika ugawaji wa tanzu za fasihi simulizi jambo ambalo linaleta mkanganyo mkubwa sana kwa wagenzi na wasomi wa fasihi simulizi. Hata hivyo mtazamao unaoelekea kuwa na mshiko zaidi ni ule wa Mulokozi ambaye anazigawa tanzu za fasihi simulizi katika aina sita ambazo ni masimulizi (hadithi), semi, ushairi, mazungumzo ya kisanaa, maigizo na ngomezi.

Utata katika uainishaji wa tanzu za fasihi simulizi
Vigezo vya uainishaji; baadhi ya wataalamu wametumia vigezo vya uainishajia mbavyo vinatofautina kati ya mwandishi mmoja na mwingine. Lakini pia watalaamu weingine kama kama vile Wamitila, (2008), mazrui & Syambo, (1992) hawajaonesha vigezo vyovyote vya uanishaji wa tanzu za fasihi simulizi jambo ambalo linaleta utata katika uainishaji kwani ni vigumu kubaini ni yupi uainishaji wake upo sahihi.
Utofauti wa Idadi katika tanzu zinazoainishwa; uainishaji wa tanzu hizi unatofautiana katika idadi wanazoainshisha wataalamu mbalimbali. Kwa mfano, Mulokozi katika jarida la Mulika Na 21 (1989) anadai kuna tanzu sita (6), Balisidya, Matteru(1987) anainisha tanzu tatu (3), Wamitila, (2008) na Okpewho, (1992) wanaainisha tanzu nne (4) za fasihi simulizi. Hivyo kutofautina kwa idadi za tanzu zinazoainishwa na watalaamu mbalimbali kunazua utata kwani ni vigumu kuhitimisha kuwa ni nani yupo sahihi.
Kuingiliana kwa tanzu; katika uainishaji wa watalamu mbalimbali baadhi ya tanzu zinaingiliana ingawa hutofautiana katika vigezo vya uainishaji wao na wengine kukosa vigezo kabisa. Hivyo basi kuingiliana kwa tanzu hizo huweza kuleta utata. Kwa mfano, Okpewho, (1992) ameainisha utanzu wa ngojera ambao unaingia katika utanzu wa ushairi kama ilivyoainishwa na Wamitila, (2008), Mulokozi, (1989). Lakini pia utanzu wa semi umeonekana katika kila uainishaji ingawa kuna utofati unaojitokeza katika uainishaji wao.
Utofauti wa isitlahi za uainishaji; baadhi ya wataalamu wametofautina katika isitilahi za uainishaji ingawa hurejelea utanzu mmoja au dhana moja. Kwa mfano, Balisidya & Matteru, (1987) anatumia istlahi nathari, Wamitila, (2008) ametumia hadithi, Okpewho, (1992) na Mulokozi, (1989) ametumia istilahi masimulizi. Tukichunguza istalahi hizo, tunapata dhana moja tu inayorejelewa na kuleta utata katika uainishaji.
Tanzu za fasihi simulizi hubadilika badilika kifani, kimaumbo na hata kimaudhui; baadhi ya tanzu za fasihi na vipera vyake huweza kubadilika kulingana na wakati. Kwa mfano utanzu wa hadithi katika kipindi cha sasa huwasilishwa tofauti na ulivyowasilishwa zamani, hivyo basi hukosa uhalithia wa hadithi kama utanzu wa fasihi simulizi kitendo ambacho waainshaji hushindwa kutengeza kigezo cha kuainisha utanzu huu.
Hivyo basi, tunahitimisha kwa kusema kuwa, fasihi simulizi kama fasihi zingine ina dhima muhimu katika jamii. Dhima za fasihi simulizi ni kama vile kuelimisha jamii, kufundisha jamii, kutabirii na kutoa mwelekeo wa jamii, kuhifadhi historia ya jamii na kuonya jamii. Pia kupitia fasihi simulizi wasimuliaji hukuza ubunifu wao kwa kutongoa masimulizi au hadithi mbalimbali. Fasihi simulizi ni chanzo kikubwa cha fasihi andishi kwani karibu vipengee au tanzu zote za fasihi andishi zimetokana na fasihi simulizi. Kwa mfano, riwaya chanzo chake ni hadithi, tamthiliya hutokana na sanaa za maonesho, semi mbalimbali za fasihi simulizi hupatikana katika fasihi andishi. Utanzu wa ushairi umetokana na ushairi simulizi ambao zamani ulikuwa ukiwasilishwa kwa uimbaji au kughani fasihi simulizi hukuza upeo wa kufikiri na ubunifu kwa hadhira kupitia elimu inayopatikana kupitia masimulizi mbalimbali.




MAREJELEO
Balisidya, M. L (1987). Tanzu na Fasihi Simulizi Katika Mulika Nambari 19. Dar es salaam:
TUKI
Kirumbi, P. S (1975). Misingi ya Fasihi Simulizi. Nairobi: Shungwaya Publishers Ltd
Mazrui, A & Syambo, B (1992). Uchambuzi wa Fasihi. Nairobi: East African Educational
Publishers.
Masebo, J. A & Nyangwine, N (2008). Nadharia ya Fasihi. Dar es salaa: Nyambari Nyangwine
Publishers.
Msokile, M (1992). Kunga za Fasihi na Lugha. Dar es salaam: DUP
Mulokozi, M. M (1989). Tanzu za Fasihi Simulizi Katika Mulika 21. Dar es salaam: TUKI
Mulokozi, M. M (1996). Utangulizi wa Fasihi Simulizi ya Kiswahili. Dar es salaam: TUKI
Ngure, A (2003). Fasihi Simulizi kwa Shule za Sekondari. Nairobi: Phoenix Publishers Ltd
TUKI, (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu (Toleo la pili). East Africa:
Oxford University Press na TUKI
Wamitila, K. W (2003). Kamusi ya Fasihi, Istilahi na Nadharia. Nairobo: Focus Publication Ltd
Wamitila, K. W (2008) Kanzi ya Fasihi: Misingi ya Uchanganuzi wa Fasihi. Nairobi: Vide-
Muwa Publishers Ltd.
Okpewho, I (1992) African Oral Literature. Backgrounds Character and Coninuity.
Bloomington: Indian University Press.

Chimbuko la Tamthiliya.


Dhana ya Tamthiliya.
Neno tamthiliya limetokana na kitenzi mithilisha kwa maana ya kufananisha au kulinganisha. Katika kiswahili, tamthiliya inatumika kwa maana ya michezo ya kuigiza. Katika tamthiliya huwa kuna ufananishaji ambapo mwigizaji hujifananisha na mhusika wa mchezo wa kuigiza.
Mazrui na Syambo (1992) wanaieleza tamthiliya kuwa ni utungo wa fasihi ambao umebuniwa kwa kiasi kikubwa kwa lugha ya mazungumzo yenye kuzua na kuendeleza matukio ya hadithi ya utungo huo.
TUKI (2004) nao wanafasili tamthiliya kuwa ni utungo wa kisanaa ambao huweka wazo fulani katika matendo na mazungumzo.
Kwa ujumla tamthiliya huweza kufasiliwa kama ni utungo wa kisanaa ambao huwasilishwa jukwaani kwa njia ya mazungumzo yanayoambatana na matendo/utendaji ambao husawiri matukio halisi katika jamii husika.
Chimbuko la Tamthiliya.
Kauli inayodai kuwa chimbuko la tamthiliya linahusishwa na tamthiliya kuzingatia sanaa au mwigo tu na kuacha matendo ya dhati si kweli kwani chimbuko la tamthiliya linahusisha pia matendo ya dhati (miviga). Tunaweza kudhihirisha chimbuko la tamthiliya duniani kote kwa kuzingatia mambo matatu ambayo ni; Miviga, Mwigo/umithilishaji pamoja na Sanaa za maonyesho.
Miviga.
Miviga ni dhana inayotumiwa kuelezea sherehe ambazo aghalabu hufanywa katika kipindi maalumu katika jamii fulani. Miviga ilihusiana na vitendo vya dhati kama ibada, matambiko, jando na unyago. Miviga hurejelea mihula miwili muhimu katika kuelzea chimbuko la sanaa za maonyesho – muhula wa mpito (liminal phase) na muhula wa liminoid.
.
Katika liminal phase; mtu wa kale katika juhudi zake za kutawala mazingira yake aligundua kuwa kuna matukio ambayo hakuyafahamu na ambayo yalimpumbaza. Baadhi ya matukio haya ni pamoja na majira, uhai, kifo, na maumbile ya dunia kama vile radi,na mafuriko. Ili kupambana na mambo hayo yaliyokuwa yakimpumbaza, aliomba msaada wa miungu kupitia ibada na kutambika. Matendo ambayo aliyaona yanafaa aliyarudiarudia hadi kuwa matendo ya kuaminika na ya kudumu yaani miviga. Matendo hayo ya dhati yalijitokeza katika sehemu mbalimbali za ulimwengu mfano katika nchi ya Ugiriki-Ulaya magharibi, matendo haya alifanyiwa Dionysus ambaye alikuwa mungu wa mvinyo na neema. Inamaanisha kuwa Dionysus alikuwa mtoto wa Zeus (mungu mkuu) na ambaye aliuawa na kufufuka. Wagiriki walilinganisha hadithi hii ya kufa na kufufuka kwa Dionysus na mzunguko wa majira kama masika ambayo yalileta neema.
Barani Afrika matukio haya yalionekana miongoni mwa makabila fulanifulani, mfano Wakamba nchini Kenya ambapo inaaminika kuwa na matambiko kwa miungu yao tangu jadi na hasa wanapokabiliwa na hali ngumu ya maisha hususani ukame na pia wanapopata neema kama mvua humshukuru mungu wao kupitia matambiko.Mfano mwingine ni kutoka kwa jamii ya Wazinza nchini Tanzania ambapo walikuwa na mungu wao aitwaye Msambwa ambapo walikuwa wakifanya matambiko yaliyoambatana na ngoma inayoitwa mlekule. Kutokana na maendeleo katika jamii mbalimbali duniani, jamii baadhi zilipiga hatua na kuendelea kutoka hatua ya liminal phase hadi muhula wa pili unaoitwa liminoid phase .
Katika kipindi cha liminoid phase; kumekuwa na mgawanyiko maalum wa kazi kama vile wakulima, wafugaji, wafua vyuma, wasanii na maseremala. Kutokana na mgawanyiko huu wa kazi, chakula cha ziada kikazalishwa ambacho kiliruhusu watu wengine kufanya sanaa za maonesho, kitendo ambacho hakizalishi na kukidhi mahitaji yao na kusababisha watu wenye uwezo kuwadhamini wasanii. Sanaa za maonesho zilikuwa hasa na lengo la kuburudisha.Watu wa aina hii (wadhamini) walipotokea walifanya chimbuko la sanaa za maonesho kufikia hatima yake na kuzaliwa kwa sanaa za maonesho yaliyokamilika yaani Tamthiliya. Hivyo tamthiliya inahusisha matendo ya dhati na yasiyo ya dhati na hayawezi kutenganishwa.


Mwigo/umilithishaji wa maisha ya kawaida.
Kwa mujibu wa Aristotle katika kitabu chake poetics anaeleza kuwa mwigo ni tendo la kufanya au kufuatisha jambo lililofanywa na mtu mwingine kabla yake au uumbaji upya wa kile kilichopo kwa ajili kukifanya bora zaidi. Aristotle aliona asili ya sanaa za maonesho inatokana na mwigo. Maandishi yake katika Poetics yalifafanua sheria au kanuni za utunzi wa tamthiliya, ambazo kwa muda mrefu sana zilichukuliwa na wanasanaa wengi wa michezo ya kuigiza kama mwongozo karibu kote ulaya. Mwigo huwepo maishani mwa binadamu kwa sababu mbalimbali kama vile; binadamu hufurahia kuiga wengine, binadamu hufurahia kuona maigizo. Mara nyingi mtu anapomuiga mtu mwingine hutenda kama yeye. Pia kuiga ni moja kati ya mbinu kubwa ya kujifunza juu ya ulimwengu wake. Kwahiyo ni dhahiri kuwa chimbuko la tamthiliya pia linahusiana kwa karibu sana na uigaji au mwigo.
Nadharia ya Sanaa za maonyesho.
Sanaa za maonyesho; ni uoneshaji wa maisha kisanaa ambapo mwoneshaji na hadhira huwepo mahali pamoja kwa wakati mmoja. Kwa mfano maonesho ya ngoma za kijadi,dansa na majigambo. Sanaa za maonesho ulimwenguni zilichipuka katika kipindi cha “liminoid phase” ambapo kulikuwa na wadhamini mbalimbali wa maonesho hayo hasa Ulaya Magharibi. Ulaya magharibi ndiyo inayosemekana kuwa ya kwanza kufikia kipindi cha “liminoid phase” kutokana na mgawanyiko wa kazi ndani ya jamii.
Tunaposema sanaa za maonesho za kijadi tuna maana ya zile ambazo zimechipuka katika jamii. Sanaa hizo ni pamoja na ngoma, majigambo, miviga, mashairi, na zingine.Hizi zilikuwa zikiambatana na lugha na matendo ya mwili. Mfano maonesho ya “dithyramb” ambayo yalikuwa maalumu kwa mungu wa Wagiriki kwa jina la “Dionysus” ndiyo hasa asili ya tamthiliya huko Ugiriki. Maonesho hayo yaliambatana na itikio (chorus) ambayo iliimba hadithi. Kadri muda ulivyokuwa unapita, itikio lilitoweka na hadithi ikawa inatambwa mfano mtambaji Arion aliziandika kwa ufasaha na huu ukawa mwanzo wa tamthiliya.
Nchini Uingereza, tamthiliya ilianza kujengeka karne ya 10-13BKM tofauti na Ugiriki ambapo tamthiliya zilianzia na maonesho aliyokuwa akifanyiwa Dionysus (mungu wao), nchini Uingereza tamthiliya zilianzia makanisani ambapo misa zilikuwa zikiigizwa (liturgical drama). Haya yalikuwa maigizo ya pasaka ya mwaka 995BKM ambayo inasemekana yaliandikwa kwa misingi ya tamthiliya. Sababu hasa ya kuigiza misa ilikuwa ni kurahisisha ili ieleweke vizuri kwa waumini. Katika maigizo haya baadhi ya sehemu za biblia pia ziliigizwa.
Baadaye nje ya Ulaya hususani Japan, mambo yalikuwa tofauti ambapo kuna drama ziitwazo“Kabuki”ambazo ni mseto wa utambaji wa hadithi, ngoma na shani (spectacle) – kichekesho.Kuna aina nyingine ya drama ya Kijapan iitwayo Noh huchanganya dansa, ushairi, muziki, uigizaji wa kawaida, seti na maleba maalumu yasiyokuwa na uhalisia ili kusawiri miviga (rituals) au matendo ya kidini.
Nchini China (Uchina) drama ilitokana na sherehe za kidini zilizotendwa na makuhani wa kibudha kwa kutumia nyimbo, dansa, na maigizo bubu. Maigizo haya kama ya Kijapan ilikuwa ni faraguzi yaani hapakuwa na mswada wa mchezo mzima bali muhtasari tu ambao ulijawa na uigizaji wenyewe wakati wa maonesho.
Maigizo yaliyokuwa yakifanyika makanisani mfano Uingereza, Uchina na Japan polepole yakaanza kutoka kanisani na kuanza kusawiri maisha ya vijijini ambapo maisha yalianza kuigizwa na huo ndio mwanzo wa tamthiliya kuingia vijijini na kuanza kuzungumzia mambo mengine tofauti na ya kidini.
Barani Afrika, chimbuko la tamthiliya linahusishwa na maigizo ya kitamthiliya ya Misri ambako michezo ya miviga iliyohusu kufa na kufufuka kwa mungu wao aliyeitwa Osiris iliyokuwa ikichezwa kwa miaka kama 2000 kuanzia mwaka 2500KM (Brockett, 1979:04) .Baadhi ya wataalamu wanakubali kuwa drama hizo za kimisri ziliathiri maigizo ya mwanzo ya Wayunani. Mbali na drama za kimisri ambazo huenda ziliandikwa, maigizo yasiyoandikwa hapa Afrika yalikuwa ni sehemu ya matendo yanayosawiri jamii hasa katika miviga ya watoto na maigizo ya watani tangu zamani.
Dhana ya sanaa ya maigizo na hata tamthiliya ikiwa na maana ya utendaji wa dhana, haikuanza tu na majilio ya wakoloni hapa Afrika. Baadhi ya ngoma, burudani, dansi, sherehe kama vile mavuno, matanga na harusi, majigambo ya kiasili na simulizi mbalimbali za Mwafrika zilizaliwa na matambiko katika jamii mbalimbali.
HISTORIA YA FASIHI YA KISWAHILI
Kwa upande wa utamaduni wa waswahili kwa mfano, kabla ya ujilio wa wageni (watu kutoka Ulaya magharibi) na kuleta drama yao, waswahili walikuwa wakitunga na kughani tendi ambazo baadhi zilipata kuandikwa kwa hati za Kiarabu. Tendi hizo ziliwasilishwa kwa namna ya maigizo, matendo na kutofautisha maneno ya wahusika mbalimbali na ya wasimulizi, masuala mbalimbali ya utamaduni wa Waswahili. Maigizo hayo hutoa maelezo kuhusu mandhari, mavazi na vifaa vingine – maelezo ambayo yanafanana na jukwaa la kisasa tunalosoma na kutumia katika michezo ya kuigiza. Drama hizi zilifungamana na fasihi simulizi, hazikuwa za kibiashara, hazikurasimishwa na hazikuandikwa.
Tamthiliya zilizoandikwa ili ziigizwe rasmi jukwaani ni matokeo ya tamhiliya za Ulaya- yaani athari za kimagharibi. Hata hivyo tamthiliya za Kiswahili zilienzi desturi na mila za kijadi pamoja na mielekeo yake. Hii hudhihirishwa kupitia miktadha iliyotumiwa na wasanii katika kazi zao. Mfano tamthiliya kama vile Kinjeketile na Mashetani(E.Hussein), Pambo (P.Muando), Mkwawa wa Uhehe (Mulokozi), Aliyeonja Pepo (C.Topan), Kilio cha Haki (Mazrui .A), Mzalendo Kimath (Ngugi wa Thiongo), na Wingu Jeusi (Chacha.N) ni vielelezo vya uhuishaji wa utamaduni na imani za asili za mwafrika.
Kwa ujumla chimbuko la tamthiliya hujumuisha sanaa za maonesho, mwigo pamoja na miviga (matendo ya dhati), ambapo miviga ilizaa sanaa za maonesho na mwigo. Hii haimanishi kuwa matendo ya dhati yalipotea bali bado yanatumika katika ujenzi wa tamthiliya kwani bado kuna jamii ambazo zipo kwenye kipindi cha mpito- yaani liminal phase, ambao bado hutumia miviga mfano Wamasai, Wakurya ,Wakamba, Wakalejin, Wasukuma, Wairaq, Wabarbaik wote wa Afrika mashariki.
Ukilinganishwa na tanzu nyingine za fasihi ya Kiswahili, utanzu wa tamthiliya ndio mchanga zaidi. Hata hivyo, chimbuko lake kwa upande wa sanaa-tendaji ni la kale mno. Chimbuko lake hasa ni katika fasihi simulizi ya Kiswahili – katika mawasilianao ya moja kwa moja baina ya msimulizi wa ngano na hadhira, katika maigizo mbalimbali ya msimulizi wa ngano, katika ushirikiano wa moja kwa moja baina ya msimulizi na hadhira yake, katika majibizano ya kishairi yanayotokea katika hafla mbalimbali, katika nyimbo na ngoma za watoto na watu wazima, katika michezo ya sarakasi na kadhalika. Kwa hiyo, historia na maendeleo ya tamthiliya nchini Tanzania inaweza kuelezwa kwa kurejelea vipindi vitatu muhimu: Kabla ya Ukoloni, Kipindi cha Ukoloni na Kipindi cha Uhuru.
KABLA YA UKOLONI
 Tamthiliya zilizoandikwa ili ziigizwe jukwaani hazikuwepo kabla ya ukoloni. Mchezo wa kuigiza ulioandikwa ulikuja na wakoloni (Bertoncini, 1989). Aina za sanaa za maonyesho zilizokuwepo zilitofautiana na tamthiliya hii iliyoingizwa na tamaduni ngeni. Zilikuwepo tamthiliya zisizoandikwa, zilizogezwa au kufaraguzwa (improvised) kwa ajili ya kuonyeshwa kwenye shughuli maalumu, kwa mfano sherehe za jando na unyago, mazishi, kutawazwa kwa mtemi, arusi na michezo ya watoto. Tamthiliya hizo zilikuwa na sifa kadha za tamthiliya, yaani hadithi, vitendo, wahusika na waigizaji wao, na dialojia. Isitoshe, zilikuwa na sifa za Sanaa za Maonyesho kama vile: Dhana Inayotendeka, Uwanja Unaotendewa, Watendaji, Hadhira, Kusudio la Kisanaa, Muktadha wa Kisanaa na Ubunifu (Umithilishaji). Tamthiliya hizo hazikuwa na ploti ya ki-Aristotle wala matini yaliyoandikwa. Hivyo hizi zilikuwa tamthiliya-simulizi.
Kipindi Cha Ukoloni (1890–1960) 
Tamthiliya ilianza Tanzania wakati ukoloni ulipoingia hasa kuanzia miaka ya 1920. Ukoloni unahusu jamii mbili ambapo jamii moja yenye nguvu huitawala jamii nyingine. Katika hali kama hii, hutokea tamaduni mbili – utamaduni unaokandamiza na ule unaokandamizwa. Katika kipindi hiki palikuwepo: Tamthiliya za Kizungu, Vichekesho naTamthiliya ya Kiswahili.
Tamthiliya za Kizungu
Tamthiliya za kizungu zilikusudiwa ama kuwaburudisha maofisa na walowezi (masetla) wa kizungu, au kufundisha Bibilia na imani ya Kikristo.Tamthiliya hizi ziliigizwa kuanzia miaka ya 1920, nyingi zilichezwa mashuleni. Shule ndio hasa zilitumika kuonyeshea tamthiliya zilizojaa ujumi, amali na itikadi ya Kibepari. Kwa sababu tamthiliya inahitaji kusomwa na kukaririwa kabla ya kuonyeshwa kwenye jukwaa, basi usomi ulikuwa kigezo kikubwa cha kufanikisha tamthiliya. Hali hii iliwafanya wala tu waliojua kusoma na kuandika Kiingereza waimudu fani hii. Hawa walipatikana shuleni tu ukiondoa wakoloni wenyewe. St. Joseph Convent School, hivi sasa Forodhani, ilianza kuonyesha tamthiliya za Kiingereza kuanzia 1922. Tamthiliya hizo ni kama vile The Sherrif’s Kitchen, The Ugly Duckling ya Milne na The Birds of a Feather ya Francis. Nyingi katika tamthiliya hizi zilikuwa zile za wakati wa Victoria huko Uingereza (1893-1914). Tamthiliya hizi zilijulikana kama ‘Drawing Room Drama’. Zilijishughulisha na masuala ya kinyumbani, yaani jinsi familia ya Kiingereza huishi, matazamio yake na mambo yafafanayo na hayo. Kwa kifupi, tamthiliya hizi zilitakiwa kuwa na ujumi-taaluma wa tamthiliya, yaani lugha na mtindo wa uonyeshaji uliotakiwa Uingereza wakati huo – ‘Four Wall-Bourgeois Theatre’Tamthiliya zote zilikuwa kwenye Kiingereza. Baadhi ya tamthiliya zilitokana na michezo iliyoandikwa na Waingereza, kwa mfano Shakespeare, na baadhi zilikuwa ni za dini ya
Kikristo.
Takriban tamthiliya zote za kipindi hiki zilikuwa ni za kibwanyenye, yaani zisizopingana na mfumo wa ubepari na ukoloni uliokuwepo. Tamthiliya chache mno zilitafsiriwa kwa Kiswahili, kwa mfano, tamthiliya ya Moliere, ‘Le Medecin Malge Lui’ “Tabibu Asiyependa Utabibu”. Mbali na shule, zilianzishwa taasisi zingine zilizojishughulisha na tamthiliya. Hindu Volunteer Corps ambayo ilionyesha tamthiliya za Kihindi ilianzishwa mnamo 1938. Baadaye, vilianzishwa vikundi vya kuigiza tamthiliya za kizungu: Dar es Salaam players (Little Theatre, 1947) na Arusha Little Theatre, 1953 (Lihamba, 1985:38). Tamthiliya katika lugha ya Kiingereza ilizidi kushamiri baada ya kufanyika mkutano wa wakoloni wa Kiingereza huko Cambridge mwaka wa 1948 uliojulikana kama ‘Cambridge Summer Conference’. Mkutano huu uliongelea suala la kutumia maonyesho kama kipengengele kimoja cha kueneza utamaduni wa Kiingereza kwenye makoloni. Kwa hiyo, matombola, brass bendi na tamthiliya vikatiliwa mkazo. Matokeo ya mkutano huu kwenye makoloni ikawa ni uanzishwaji wa mashindano ya tamthiliya shuleni. Mnamo mwaka wa 1957, Baraza la Kiingereza (British Council) lilianzisha mashindano ya uigizaji wa tamthiliya za Kiingereza nchini Tanzania, yaliyoitwa ‘School Drama
Competition’. Tamthiliya zote zilibidi kuwa kwenye lugha fasaha ya Kiingereza. Mashindano hayo yaliendelea hadi 1963, yalipoanza kusimamiwa na Youth Drama Association. Kuanzia wakati huo, tamthliya za Kiswahili zilianza kuhusishwa katika mashindano hayo, na hivyo kuchochea utuzi wa tamthiliya katika lugha hiyo.
Vichekesho
Vichekesho1 ni aina ya tamthiliya-gezwa (zilizotungwa papo kwa hapo bila kuandikwa). Zilianza miaka ya 1920 kwa lengo la kuburudisha wenyeji. Tamthiliya hizo kwa kawaida zilikuwa na vituko vya kuchekesha na ziliwasuta watu waliofikiriwa kuwa ‘washamba’, ‘wajinga’ au ‘wasiostaarabika’. Tamthiliya hizo zilimwonyesha mhusika anayetoka shamba na kwenda kuzuzuka mjini. Vichekesho viliendelea hata baada ya uhuru (na bado vipo) ila dhamira
zake zilibailika.
Tamthiliya-Andishi ya Kiswahili

 Kipindi cha Uhuru

Tamthiliya ya Kizungu
Tamthiliya ya kizungu iliendelea kuigizwa hata baada ya uhuru, hasa mashuleni na katika kumbi maalumu za maonyesho kama Little Theatres. Hata hivyo, umaarufu wake ulipungua kiasi, hususan upande wa Tanzania. Baadhi ya tamtiliya muhimu za kizungu zilianza kutafsiriwa na kuigizwa kwa lugha ya Kiswahili ili zieleweke zaidi na wananchi km. tafsiri za J.K. Nyerere za Shakespeare, Juliasi Kaisari (OUP, 1964) na Mabepari wa Venisi (OUP, 1969); tafsiri za S.S. Mushi za michezo ya Shakespeare ya Makbeth (TPH, 1968) na Tufani (TPH, 1969); Moliere, Mchuuzi Muungwana (A. Morrison, EALB 1961) na Mnafiki (L. Taguaba, TPH 1973); Sophocles, Mfalme Edipode (S.S. Mushi OUP, 1971); Gogol, Mkaguzi Mkuu wa Serikali (C. Mwakasaka, HEB 1979), nk. Licha ya tamthiliya za kizungu, kadhalika tamthiliya za Kiafrika zilizoandikwa kwa lugha za kigeni na lugha nyingine za kiafrika, zilifasiriwa kwa Kiswahili km. Mtawa Mweusi (Ngugi wa Thiong’o, HEB, 1978); Soyinka W. Masaibu ya Ndugu Jero (Mf. A.S. Yahya OUP 1974); O. Ijimere, Kifungo cha Obatala (HEB, 1978); Ngugi wa Thing’o na Ngugi Mirii, Nitaolewa Nikipenda (HEB, 1982); M. Mulokozi (1968), The Tragedy of Mkwawa (Mf. Kahingi, 1970).

Vichekesho
Baada ya uhuru vichekesho vilichua sura tofauti kidogo. Badala ya kuwasuta ‘washamba’ vilianza kuwasuta ‘wazungu weusi’, yaani waafrika wanaoringia elimu au vyeo na kudharau utamaduni wao (Darlite 2/2: 133-152). Vipengele kama matendo, maonyesho na maongezi vilitumiwa katika uundaji wa vichekesho hivi. Baadhi ya vichekesho, hasa vinavyoonyeshwa kwenye mabaa na sehemu nyingine za burudani na starehe, hujaribu kuzungumzia matatizo ya watu wa kawaida, km. matatizo ya familia, ukosefu wa kazi, ukimwi, uhalifu, udanganyifu wa waganga wa jadi, nk.Vipo pia vichekesho vya kisiasa vyenye kuzungumzia kadhia za kisiasa, ubinafsi wa viongozi, matatizo yanayokumba watu vijijini, mijini, nk. Baadhi ya vichekesho vya redio Tanzania, km. “Mahoka” (kipindi kilichoanza mwaka 1974) na “Pwagu na Pwaguzi” (kilianza mwaka 1978), hukejeli na kukemea tabia mbovu za baadhi ya watu, wakiwemo viongozi wa kiasa. Siku hizi vichekesho hutangazwa na vituo vya redio na televisheni, na huonyeshwa mijini kwenye kumbi za starehe.
 Tamthiliya-Andishi ya Kiswahili
Baada ya uhuru utunzi wa tamthiliya ulipamba moto zaidi, hasa upande wa Tanzania. Uhuru uliwafanya waandishi wa tamthiliya kuandika mambo ambayo wasingeweza kuyaandika hapo awali. Waandishi walitumia tamthiliya kuelezea matatizo yanayokabili jamii. Mashindano ya utunzi na uigizaji yaliyoendeshwa na Youth Drama Association nchini Tanzania yaliwawezesha watunzi chipukizi kujitokeza, akiwemo Ebrahim Hussein ambaye tamthiliya yake ya kwanza, Wakati Ukuta (EAPH,1969) ilishinda tuzo katika mashindano hayo. Wengine walikuwa Uhinga na Katalambula ambao walitunga tamthiliya za Kiswahili zilizoonyesha maadili katika jamii. Wakati huo pia ndipo walipoanza kutokea watunzi waliohitimu fani ya sanaa za maonyesho katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam km. E. Hussein, P. Muhando, N. Ngahyoma na G. Uhinga. Kwa mujibu wa Mulama (1983) watunzi walianza kuifungamanisha tamthiya na mahitaji ya nchi ya Tanzania. Uzukaji wa tamthiliya ukaambatana na hali maalumu za kiuchumi na kijamii.

MAREJELEO.

Dhana na historia ya sarufi mapokeo


Dhana ya Sarufi
Sarufi ni kanuni, sheria au taratibu zinazotawala lugha katika matumizi yake ambayo hujumuisha matamshi, maumbo, miundo na maana (Saluhaya, 2010:72).
Massamba na wenzake (1999) Sarufi ni kanuni, sheria au taratibu zinazotawala kila moja kati ya viwango vinne vya lugha ambavyo ni umbo-sauti (fonolojia), umbo-neno (mofolojia), miundo maneno (sintaksia) na umbo maana (semantiki).
Matinde (2012:211) Sarufi ni taaluma ya lugha inayochunguza na kuchanganua vipashio na kanuni mbalimbali zinazotawala muundo wa lugha.
Massamba (2004) anasema, sarufi ni taaluma ya lugha inayohusu uchunguzi na uchanganuzi wa kanuni za vipengele mbalimbali vya lugha.
Kwa ujumla sarufi inaweza kuelezwa kama kanuni, sheria na taratibu zinazomuongoza mzungumzaji au mwandishi kuzungumza au kuandika tungo sahihi zinzoeleweka kwa msikilizaji wa lugha ileile. Kama ni mzawa wa lugha, mtumiaji huwa tayari anazo kanuni hizo (hata katika uzungumzaji), yaani kanuni anakuwa nazo akilini baada ya kusomaau kuishi na watu wa lugha hiyo.
Dhana na historia ya sarufi mapokeo
Kwa mujibu wa Massamba na wenzake (1999) wanaeleza kuwa, sarufi mapokeo ni sarufi elekezi ikisisitiza usahihi wa lugha kwa kuonesha sheria ambazo hazina budi kufuatwa, mathalani kufanya muundo fulani wa sentensi usomeke kwa usahihi au sheria ambazo hazina budi kufuatwa ili kufanya matamshi fulani yakubalike kuwa ndio sahihi.
Matinde (2012:211) anaeleza kuwa, mkabala huu wa sarufi mapokeo ni mkabala wa awali ulioshughulikia sarufi ya lugha. Waasisi wake walikuwa wanafalsafa wa Ugiriki. Habwe na Karanja (2004:129) anataja wanafalsafa hao kuwa ni Plato, Aristotle, Dionysus Thrax, na Priscian. Katika kipindi hiki sarufi ilishughulikiwa sambamba na falsafa, dini, fasihi, balagha na mantiki. Plato alikuwa wa kwanza kugawa sentensi katika sehemu kuu mbili mtenda (subject) na kitendwa (object). Hatimaye Aristotle akaendeleza kazi ya mwalimu wake kwa kugawa sentensi katika sehemu kuu tano ambazo pia ndizo aina za maneno; nomino, kitenzi, kivumishi, kiunganishi na kielezi.
Miaka ya 100 K.K, mwanasarufi Myunani Dionysus Thrax aliandika kitabu cha sarufi ambacho ni cha awali kabisa kilichoitwa “Techne Grammatike (The Art of Grammar)”. Mwanasarufi huyu aliainisha sehemu saba za sentensi ambazo ni nomino, kitenzi, kivumishi, kiwakilishi, kiunganishi, kielezi na kiingizi.
Dhana ya Neno
Habwe na Karanja (2007:71) wanafafanua kuwa, neno ni kipashio cha kiisimu kinachoundwa na mofimu moja au zaidi.
Saluhaya (2010:135) anadai kuwa, neno ni mkusanyiko wa sauti zinazotamkwa au kuandikwa kwa pamoja na kuleta maana.
Massamba na wenzake (1999:43) katika samikisa wakitilia maanani maelezo ya Lyons (1968:194-208), neno linaweza kufafanuliwa katika misingi ya kiumbo-sauti (yaani, kwa kuchunguza sauti zinazounda umbo zima), kiothografia (yaani kwa kuchunguza herufi zinazotumika katika kuliandika umbo hilo), na kisarufi (yaani kwa kuchunguza kile kinachowakilishwa na umbo husika katika lugha).
Hivyo basi, tunaweza kufasili neno kama silabi au mkusanyiko wa silabi (sauti) unaoandikwa au kutamkwa ili kuleta maana. Maana hiyo yaweza kuwa kamili, yaani inayotoa taarifa kamili au isiwe kamili, yaani ambayo haitoi taarifa kamili kwa msomaji au msikilizaji.
Dhana ya Sentensi
Matinde (2012:157) anafafanua sentensi kuwa ni neno au fungu la maneno lenye uarifishaji mkamilifu. Sentensi huwa na muundo uliokamilika na hujitegemea kimaana.
Kwa ujumla sentensi ni kipashio kikuu katika tungo chenye uwezo wa kutoa taarifa iliyo kamili au isiyo kamili na huwa na muundo wa kiima na kiarifu.


Ufafanuzi wa aina za maneno kwa mujibu wa wanasarufi wa kimapokeo
Wataalamu wengi wa sarufi ya Kiswahili sanifu wanaelekea kukubaliana kwamba katika lugha hii kuna aina za maneno zisizopungua saba. Aina hizi za maneno zimewahi kujadiliwa kwa kina katika vitabu kadhaa vya sarufi vinavyojishughulisha na sarufi miundo na sarufi maumbo. Baadhi ya wataalamu wa sarufi mapokeo waliojadili aina hizo ni Kapinga (1983), Nkwera, Tumi, Mohamed, Massamba na wenzake (1999) na Kihore na wenzake (1999). Aina hizo ni pamoja na:
Nomino
Nomino ni jina linalotaja kitu, kiumbe, hali, dhana au tendo lolote liwalo. Tukiyachunguza kwa makini maelezo haya tunaona kwamba yanaashiria kuwa katika uamilifu wake nomino hufanya kazi ya kukipambanua au kukibainisha kitajwa kwa madhumuni ya kukitofautisha na vitajwa vingine. Kwahiyo nomino si mtajwa tu bali pia ni mtajwa bainishi.
Katika sarufi za kimapokeo, nomino zilijulikana kama majina lakini katika sarufi za kisiku hizi neno jina au majina limeonekana kuwa la kawaida mno na kwamba haliwezi kuwa na mashiko yenye kukidhi mahitajio ya kiistilahi. Kwahiyo neno nomino limependekezwa litumike badala yake (Massamba na wenzake, 1999:39 katika samikisa. Wanasarufi mapokeo wameweka migawanyo ya nomino kama ifuatavyo:
a) Nomino jumuishi - hizi ni nomino zinazohusu majina ambayo hayakibainishi wazi kitu kinachotajwa. Kwa mfano mbuzi, gari, chuo, mtu, kalamu na nyumba.
b) Nomino mahususi – ni yale majina ambayo yanataja vitu, dhana, na viumbe fulani maalumu na kwa kutoa ubainishi ambao ni wa wazi zaidi. Baadhi ya nomino mahususi ni kama vile Masalu, Ijumaa, Februari, Mwanza, Mariam, Herman, Viktoria, Tanzania na Rufiji.
c) Nomino kikundi – hizi ni nimino ambazo huhusu majina yanayotaja vikundi kadhaa vya viumbe. Katika nomino hizi, jina moja huwa linataja jumuiya yenye sifa za namna moja. Kwa mfano baraza, jeshi, familia, shule, bunge, genge, mahakama, kombania na kwaya.
d) Nomino dhahania – ni nomino zinazohusu majina ya vitu, dhana, na viumbe ambavyo kiukweli tunaweza kuviona katika akili tu lakini hatuwezi kuvibainisha kwa macho. Kwa mfano Uchawi, uzee, malaika, mizimu, Mungu ,usingizi na uchovu.
e) Nomino mguso – ni nomino zinazohusu majina ya vitu ambavyo tunaweza kuviona kwa macho na kuvitambua katika uyakinifu wake, na utambumbuzi huu huweza kutokana na kuvigusa, kuvishika au kuvionja kama vile asali, chumvi, kiti, tofali, na tonge.
f) Nomino za hesabu – hili ni kundi la nomino ambalo hutumia kigezo cha uwezekano wa kuhesabika katika uainishaji wake. Hapa tunatofautisha kati ya nomino zinazowakilisha vitu vinavyohesabika na vile visivyohesabika. Nomino za vitu vinavyohesabika ni kama vile watoto, vitu, visu, mifuko na viatu. Nomino zisizohesabika hurejelea vitu ambavyo hutokea kwa wingi na haviwezi kugawika, kwa mfano makamasi, mafuta, maji, matope, sukari, mchanga, uji, na nywele.
Vitenzi.
Ni aina ya neno linalotoa taarifa juu ya tendo linalofanyika au linalotendwa na kiumbe au kitu. Wanasarufi mapokeo wamevigawa vitenzi katika aina kuu tatu ambazo ni:
a) Kitenzi kikuu – ni kitenzi ambacho kinaweza kujitokeza peke yake katika sentensi. Mfano anakula, anampiga, tunacheza, wamechoka na anaimba.
b) Kitenzi kisaidizi – ni kitenzi ambacho kinaandamana na kitenzi kikuu katika sentensi. Kwa mfano alikuwa analima, tunapenda kusoma, na amechoka kucheza. Hivyo, maneno yaliyo katika hati mlazo ni vitenzi visaidizi.
c) Kitenzi kishirikishi – ni kile cha umbo ni na si ambacho kinachukuliwa kuwa kinashirikisha vipashio vingine katika sentensi. Kwa mfano Kahigi ni mwalimu bora, huyu msichana si mwerevu.
Vuvumishi.
Ni kipashio ambacho hutoa maelezo zaisi juu ya nomino au kiwakilishi chake. Maelezo kama hayo kwa kawaida huwa namna au jinsi nomino ilivyo, yaani inavyoonekana, inavyofikiriwa, tabia, au idadi yake. Mfano wa vivumishi ni kama vile chafu, dogo, refu, vivu, zuri, embamba, na fupi. Vivumishi vimeweza kugawanywa katika aina kuu zifuatazo:
a) Vivumishi vya sifa – ni vivumishi vinavyotaja tabia au namna vitu vilivyo au vinavyoonekana. Kwa mfano ema, nyenyekevu, pole na katili.
b) Vivumishi vya idadi – ni vivumishi vinavyoonesha jumla au hesabu ya vitu. Aina hii ya vivumishi tunaweza kuigawa katika makundi mawili ambayo ni kundi linaloonesha idadi kwa jumla na kundi linaloonesha idadi kwa hesabu. Kwa mfano ingi, chache, haba na kidogo vilievile tano, tisini, elfu , milioni na tatu.
c) Vivumishi viulizi – ni vivumishi vinavyouliza maswali kuhusiana na nomino inayoandamana navyo. Mfano watu wangapi, miti mingapi, mayai mangapi, watoto wangapi, na viti vingapi.
d) Vivumishi vya pekee – ni maumbo enye na enyewe ambayo katika Kiswahili ndiyo tu huchanganya aina na viambishi vya upatanisho wa kisarufi vinavyojitokeza navyo kimatumizi. Mfano m-tu m-refu, m-ti mrefu, miti mirefu.
Viwakilishi.
Ni aina mojawapo ya maneno katika sarufi ya lugha ambayo uamilifu wake ni kuwakilisha nomino katika miktadha mbalimbali. Kwa mfano viwakilishi nafsi, viwakilishi viashirii, viwakilishi viulizi, viwakilishi vimikilishi, viwakilishi vya idadi na viwakilishi jumla.
Viunganishi.
Ni neno linalotumika kuviweka pamoja vipashio mbalimbali ili kuvifanya viwe kipashio kikuu kimoja. Kwa mfano na, au, wala, na lakini katika sentensi zifuatazo:
Baba na Mama wanalima.
Unapenda chai au uji.
Hana huruma wala upendo.
Wanasarufi mapokeo wamevigawa viunganishi katika makundi makuu mawili kwa kuzingatia msingi wa kimaana kama vile viunganishi vya hadhi sawa na viunganishi vihusishi.
Vielezi.
Ni neno linalotumika kuelezea zaidi juu ya kitenzi. Mfano sana, mno, kabisa, polepole, harakaharaka, zaidi, sawasawa na barabara. Wanasarufi mapokeo wameviainisha vielezi katika aina kuu mbili yaani vielezi halisi na vielezi viingizi. Mfano wa vilelezi halisi ni kama vile mno, sana, bure, hasa, kabisa, ovyo, haraka na sasa. Kwa upande wa vielezi viingizi ni kama vile pu, mwa, na bwe .
Viingizi.
Ni aina ya maneno inayodokeza hisia za msemaji kama vile ya hali yake ya kufurahi, kushangaa, kushtuka, na uchungu. Haya ni maneno kama vile Lo! Alaa! Lahaula! na Aa! Maneno kama haya kwa kawaida huwa yanatumika kabla ya sentensi na aghalabu huwa hayana mfungamano wa kisarufi na sentensi inayofuata. Aina hii ya neno pia huitwa vihisishi. Jina vihisishi limekitwa zaidi katika misingi ya kimaana yaani linahusu zaidi hisia mbalimbali zinazobebwa na maneno hayo. Viingizi navyo vimegawanywa katika makundi mawili nayo ni viingizi halisi na viingizi vya taswira.
Ufafanuzi wa aina za sentensi kwa mujibu wa wanasarufi mapokeo.
Kwa upande wa sentensi, wanasarufi mapokeo wanaainisha aina tatu za sentensi kwa kuzingatia uamilifu wake. Aina hizo ni kama zifuatazo:
i) Sentensi taarifa – hizi ni sentensi zenye kutoa taarifa fulani.
Kwa mfano: Kiranja amechelewa kufika shuleni.
Kahigi kaandika kitabu cha sarufi ya Kiswahili.
ii) Sentensi ulizi – aina hii ya sentensi huwa ina pengo katika sehemu yake ya taarifa. Sentensi hizi hutaka kupata taarifa fulani.
Kwa mfano: Adam ameweza kucheza mpira?
Kalamu yako ni ipi?
iii) Sentensi Agizi – aina hii ya sentensi humuingiza msikilizaji kutenda kitendo fulani. Aghalabu sentensi ya aina hii haina sehemu ya kiima.
Kwa mfano: Toka nyuma uende mbele.
Mwite kiranja wako.
Kwa ujumla, wanasarufi mapokeo kwa kiasi fulani wanatofautiana katika uainishaji wa aina za maneno kwani kuna wengine wametaja aina kumi za maneno badala ya saba. Kwa mfano Habwe na Karanja (2004:130-139) wao wanaainisha aina kumi za maneno ambazo ni nomino, vitenzi, viwakilishi, vivumishi, vielezi, vihusishi, viunganishi, vionyeshi, vihisishi na vibainishi. Hivyo ni vigumu kutambua idadi halisi ya aina za maneno kwa mujibu wa sarufi mapokeo.



MAREJELEO.
Habwe, J. & Karanja, P. (2004). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili.Nairobi: Phoenix Publishers.
Habwe, J. & Karanja, P. (2007). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili.Nairobi: Phoenix Publishers.
Kapinga, M.C. (1983). Sarufi Maumbo ya Kiswahili Sanifu. Dar es Saalam: TUKI.
Massamba, D.P.B na Wenzake (1999). Sarufi Miundo ya Kiswahili Sanifu (SAMIKISA); Sekondari na Vyuo. Dar es Saalam: TUKI.
Matinde, R.S. (2012). Dafina ya Lugha, Isimu na Nadharia; Kwa Sekondari, Vyuo vya Kati na Vyuo Vikuu. Mwanza: Serengeti Educational Publishers (T) LTD.




hakiki na tuma maoni au mapendekezo kuhusu makala hii ya andiko langu la uchunguandiko langu

ANDIKO LA UCHUNGU (Kwa shemeji zangu na wanangu)           NYAMBUYA OGUCHU,                            S.L.P 777666,       ...