Monday, August 1, 2016

Chimbuko la Tamthiliya.


Dhana ya Tamthiliya.
Neno tamthiliya limetokana na kitenzi mithilisha kwa maana ya kufananisha au kulinganisha. Katika kiswahili, tamthiliya inatumika kwa maana ya michezo ya kuigiza. Katika tamthiliya huwa kuna ufananishaji ambapo mwigizaji hujifananisha na mhusika wa mchezo wa kuigiza.
Mazrui na Syambo (1992) wanaieleza tamthiliya kuwa ni utungo wa fasihi ambao umebuniwa kwa kiasi kikubwa kwa lugha ya mazungumzo yenye kuzua na kuendeleza matukio ya hadithi ya utungo huo.
TUKI (2004) nao wanafasili tamthiliya kuwa ni utungo wa kisanaa ambao huweka wazo fulani katika matendo na mazungumzo.
Kwa ujumla tamthiliya huweza kufasiliwa kama ni utungo wa kisanaa ambao huwasilishwa jukwaani kwa njia ya mazungumzo yanayoambatana na matendo/utendaji ambao husawiri matukio halisi katika jamii husika.
Chimbuko la Tamthiliya.
Kauli inayodai kuwa chimbuko la tamthiliya linahusishwa na tamthiliya kuzingatia sanaa au mwigo tu na kuacha matendo ya dhati si kweli kwani chimbuko la tamthiliya linahusisha pia matendo ya dhati (miviga). Tunaweza kudhihirisha chimbuko la tamthiliya duniani kote kwa kuzingatia mambo matatu ambayo ni; Miviga, Mwigo/umithilishaji pamoja na Sanaa za maonyesho.
Miviga.
Miviga ni dhana inayotumiwa kuelezea sherehe ambazo aghalabu hufanywa katika kipindi maalumu katika jamii fulani. Miviga ilihusiana na vitendo vya dhati kama ibada, matambiko, jando na unyago. Miviga hurejelea mihula miwili muhimu katika kuelzea chimbuko la sanaa za maonyesho – muhula wa mpito (liminal phase) na muhula wa liminoid.
.
Katika liminal phase; mtu wa kale katika juhudi zake za kutawala mazingira yake aligundua kuwa kuna matukio ambayo hakuyafahamu na ambayo yalimpumbaza. Baadhi ya matukio haya ni pamoja na majira, uhai, kifo, na maumbile ya dunia kama vile radi,na mafuriko. Ili kupambana na mambo hayo yaliyokuwa yakimpumbaza, aliomba msaada wa miungu kupitia ibada na kutambika. Matendo ambayo aliyaona yanafaa aliyarudiarudia hadi kuwa matendo ya kuaminika na ya kudumu yaani miviga. Matendo hayo ya dhati yalijitokeza katika sehemu mbalimbali za ulimwengu mfano katika nchi ya Ugiriki-Ulaya magharibi, matendo haya alifanyiwa Dionysus ambaye alikuwa mungu wa mvinyo na neema. Inamaanisha kuwa Dionysus alikuwa mtoto wa Zeus (mungu mkuu) na ambaye aliuawa na kufufuka. Wagiriki walilinganisha hadithi hii ya kufa na kufufuka kwa Dionysus na mzunguko wa majira kama masika ambayo yalileta neema.
Barani Afrika matukio haya yalionekana miongoni mwa makabila fulanifulani, mfano Wakamba nchini Kenya ambapo inaaminika kuwa na matambiko kwa miungu yao tangu jadi na hasa wanapokabiliwa na hali ngumu ya maisha hususani ukame na pia wanapopata neema kama mvua humshukuru mungu wao kupitia matambiko.Mfano mwingine ni kutoka kwa jamii ya Wazinza nchini Tanzania ambapo walikuwa na mungu wao aitwaye Msambwa ambapo walikuwa wakifanya matambiko yaliyoambatana na ngoma inayoitwa mlekule. Kutokana na maendeleo katika jamii mbalimbali duniani, jamii baadhi zilipiga hatua na kuendelea kutoka hatua ya liminal phase hadi muhula wa pili unaoitwa liminoid phase .
Katika kipindi cha liminoid phase; kumekuwa na mgawanyiko maalum wa kazi kama vile wakulima, wafugaji, wafua vyuma, wasanii na maseremala. Kutokana na mgawanyiko huu wa kazi, chakula cha ziada kikazalishwa ambacho kiliruhusu watu wengine kufanya sanaa za maonesho, kitendo ambacho hakizalishi na kukidhi mahitaji yao na kusababisha watu wenye uwezo kuwadhamini wasanii. Sanaa za maonesho zilikuwa hasa na lengo la kuburudisha.Watu wa aina hii (wadhamini) walipotokea walifanya chimbuko la sanaa za maonesho kufikia hatima yake na kuzaliwa kwa sanaa za maonesho yaliyokamilika yaani Tamthiliya. Hivyo tamthiliya inahusisha matendo ya dhati na yasiyo ya dhati na hayawezi kutenganishwa.


Mwigo/umilithishaji wa maisha ya kawaida.
Kwa mujibu wa Aristotle katika kitabu chake poetics anaeleza kuwa mwigo ni tendo la kufanya au kufuatisha jambo lililofanywa na mtu mwingine kabla yake au uumbaji upya wa kile kilichopo kwa ajili kukifanya bora zaidi. Aristotle aliona asili ya sanaa za maonesho inatokana na mwigo. Maandishi yake katika Poetics yalifafanua sheria au kanuni za utunzi wa tamthiliya, ambazo kwa muda mrefu sana zilichukuliwa na wanasanaa wengi wa michezo ya kuigiza kama mwongozo karibu kote ulaya. Mwigo huwepo maishani mwa binadamu kwa sababu mbalimbali kama vile; binadamu hufurahia kuiga wengine, binadamu hufurahia kuona maigizo. Mara nyingi mtu anapomuiga mtu mwingine hutenda kama yeye. Pia kuiga ni moja kati ya mbinu kubwa ya kujifunza juu ya ulimwengu wake. Kwahiyo ni dhahiri kuwa chimbuko la tamthiliya pia linahusiana kwa karibu sana na uigaji au mwigo.
Nadharia ya Sanaa za maonyesho.
Sanaa za maonyesho; ni uoneshaji wa maisha kisanaa ambapo mwoneshaji na hadhira huwepo mahali pamoja kwa wakati mmoja. Kwa mfano maonesho ya ngoma za kijadi,dansa na majigambo. Sanaa za maonesho ulimwenguni zilichipuka katika kipindi cha “liminoid phase” ambapo kulikuwa na wadhamini mbalimbali wa maonesho hayo hasa Ulaya Magharibi. Ulaya magharibi ndiyo inayosemekana kuwa ya kwanza kufikia kipindi cha “liminoid phase” kutokana na mgawanyiko wa kazi ndani ya jamii.
Tunaposema sanaa za maonesho za kijadi tuna maana ya zile ambazo zimechipuka katika jamii. Sanaa hizo ni pamoja na ngoma, majigambo, miviga, mashairi, na zingine.Hizi zilikuwa zikiambatana na lugha na matendo ya mwili. Mfano maonesho ya “dithyramb” ambayo yalikuwa maalumu kwa mungu wa Wagiriki kwa jina la “Dionysus” ndiyo hasa asili ya tamthiliya huko Ugiriki. Maonesho hayo yaliambatana na itikio (chorus) ambayo iliimba hadithi. Kadri muda ulivyokuwa unapita, itikio lilitoweka na hadithi ikawa inatambwa mfano mtambaji Arion aliziandika kwa ufasaha na huu ukawa mwanzo wa tamthiliya.
Nchini Uingereza, tamthiliya ilianza kujengeka karne ya 10-13BKM tofauti na Ugiriki ambapo tamthiliya zilianzia na maonesho aliyokuwa akifanyiwa Dionysus (mungu wao), nchini Uingereza tamthiliya zilianzia makanisani ambapo misa zilikuwa zikiigizwa (liturgical drama). Haya yalikuwa maigizo ya pasaka ya mwaka 995BKM ambayo inasemekana yaliandikwa kwa misingi ya tamthiliya. Sababu hasa ya kuigiza misa ilikuwa ni kurahisisha ili ieleweke vizuri kwa waumini. Katika maigizo haya baadhi ya sehemu za biblia pia ziliigizwa.
Baadaye nje ya Ulaya hususani Japan, mambo yalikuwa tofauti ambapo kuna drama ziitwazo“Kabuki”ambazo ni mseto wa utambaji wa hadithi, ngoma na shani (spectacle) – kichekesho.Kuna aina nyingine ya drama ya Kijapan iitwayo Noh huchanganya dansa, ushairi, muziki, uigizaji wa kawaida, seti na maleba maalumu yasiyokuwa na uhalisia ili kusawiri miviga (rituals) au matendo ya kidini.
Nchini China (Uchina) drama ilitokana na sherehe za kidini zilizotendwa na makuhani wa kibudha kwa kutumia nyimbo, dansa, na maigizo bubu. Maigizo haya kama ya Kijapan ilikuwa ni faraguzi yaani hapakuwa na mswada wa mchezo mzima bali muhtasari tu ambao ulijawa na uigizaji wenyewe wakati wa maonesho.
Maigizo yaliyokuwa yakifanyika makanisani mfano Uingereza, Uchina na Japan polepole yakaanza kutoka kanisani na kuanza kusawiri maisha ya vijijini ambapo maisha yalianza kuigizwa na huo ndio mwanzo wa tamthiliya kuingia vijijini na kuanza kuzungumzia mambo mengine tofauti na ya kidini.
Barani Afrika, chimbuko la tamthiliya linahusishwa na maigizo ya kitamthiliya ya Misri ambako michezo ya miviga iliyohusu kufa na kufufuka kwa mungu wao aliyeitwa Osiris iliyokuwa ikichezwa kwa miaka kama 2000 kuanzia mwaka 2500KM (Brockett, 1979:04) .Baadhi ya wataalamu wanakubali kuwa drama hizo za kimisri ziliathiri maigizo ya mwanzo ya Wayunani. Mbali na drama za kimisri ambazo huenda ziliandikwa, maigizo yasiyoandikwa hapa Afrika yalikuwa ni sehemu ya matendo yanayosawiri jamii hasa katika miviga ya watoto na maigizo ya watani tangu zamani.
Dhana ya sanaa ya maigizo na hata tamthiliya ikiwa na maana ya utendaji wa dhana, haikuanza tu na majilio ya wakoloni hapa Afrika. Baadhi ya ngoma, burudani, dansi, sherehe kama vile mavuno, matanga na harusi, majigambo ya kiasili na simulizi mbalimbali za Mwafrika zilizaliwa na matambiko katika jamii mbalimbali.
HISTORIA YA FASIHI YA KISWAHILI
Kwa upande wa utamaduni wa waswahili kwa mfano, kabla ya ujilio wa wageni (watu kutoka Ulaya magharibi) na kuleta drama yao, waswahili walikuwa wakitunga na kughani tendi ambazo baadhi zilipata kuandikwa kwa hati za Kiarabu. Tendi hizo ziliwasilishwa kwa namna ya maigizo, matendo na kutofautisha maneno ya wahusika mbalimbali na ya wasimulizi, masuala mbalimbali ya utamaduni wa Waswahili. Maigizo hayo hutoa maelezo kuhusu mandhari, mavazi na vifaa vingine – maelezo ambayo yanafanana na jukwaa la kisasa tunalosoma na kutumia katika michezo ya kuigiza. Drama hizi zilifungamana na fasihi simulizi, hazikuwa za kibiashara, hazikurasimishwa na hazikuandikwa.
Tamthiliya zilizoandikwa ili ziigizwe rasmi jukwaani ni matokeo ya tamhiliya za Ulaya- yaani athari za kimagharibi. Hata hivyo tamthiliya za Kiswahili zilienzi desturi na mila za kijadi pamoja na mielekeo yake. Hii hudhihirishwa kupitia miktadha iliyotumiwa na wasanii katika kazi zao. Mfano tamthiliya kama vile Kinjeketile na Mashetani(E.Hussein), Pambo (P.Muando), Mkwawa wa Uhehe (Mulokozi), Aliyeonja Pepo (C.Topan), Kilio cha Haki (Mazrui .A), Mzalendo Kimath (Ngugi wa Thiongo), na Wingu Jeusi (Chacha.N) ni vielelezo vya uhuishaji wa utamaduni na imani za asili za mwafrika.
Kwa ujumla chimbuko la tamthiliya hujumuisha sanaa za maonesho, mwigo pamoja na miviga (matendo ya dhati), ambapo miviga ilizaa sanaa za maonesho na mwigo. Hii haimanishi kuwa matendo ya dhati yalipotea bali bado yanatumika katika ujenzi wa tamthiliya kwani bado kuna jamii ambazo zipo kwenye kipindi cha mpito- yaani liminal phase, ambao bado hutumia miviga mfano Wamasai, Wakurya ,Wakamba, Wakalejin, Wasukuma, Wairaq, Wabarbaik wote wa Afrika mashariki.
Ukilinganishwa na tanzu nyingine za fasihi ya Kiswahili, utanzu wa tamthiliya ndio mchanga zaidi. Hata hivyo, chimbuko lake kwa upande wa sanaa-tendaji ni la kale mno. Chimbuko lake hasa ni katika fasihi simulizi ya Kiswahili – katika mawasilianao ya moja kwa moja baina ya msimulizi wa ngano na hadhira, katika maigizo mbalimbali ya msimulizi wa ngano, katika ushirikiano wa moja kwa moja baina ya msimulizi na hadhira yake, katika majibizano ya kishairi yanayotokea katika hafla mbalimbali, katika nyimbo na ngoma za watoto na watu wazima, katika michezo ya sarakasi na kadhalika. Kwa hiyo, historia na maendeleo ya tamthiliya nchini Tanzania inaweza kuelezwa kwa kurejelea vipindi vitatu muhimu: Kabla ya Ukoloni, Kipindi cha Ukoloni na Kipindi cha Uhuru.
KABLA YA UKOLONI
 Tamthiliya zilizoandikwa ili ziigizwe jukwaani hazikuwepo kabla ya ukoloni. Mchezo wa kuigiza ulioandikwa ulikuja na wakoloni (Bertoncini, 1989). Aina za sanaa za maonyesho zilizokuwepo zilitofautiana na tamthiliya hii iliyoingizwa na tamaduni ngeni. Zilikuwepo tamthiliya zisizoandikwa, zilizogezwa au kufaraguzwa (improvised) kwa ajili ya kuonyeshwa kwenye shughuli maalumu, kwa mfano sherehe za jando na unyago, mazishi, kutawazwa kwa mtemi, arusi na michezo ya watoto. Tamthiliya hizo zilikuwa na sifa kadha za tamthiliya, yaani hadithi, vitendo, wahusika na waigizaji wao, na dialojia. Isitoshe, zilikuwa na sifa za Sanaa za Maonyesho kama vile: Dhana Inayotendeka, Uwanja Unaotendewa, Watendaji, Hadhira, Kusudio la Kisanaa, Muktadha wa Kisanaa na Ubunifu (Umithilishaji). Tamthiliya hizo hazikuwa na ploti ya ki-Aristotle wala matini yaliyoandikwa. Hivyo hizi zilikuwa tamthiliya-simulizi.
Kipindi Cha Ukoloni (1890–1960) 
Tamthiliya ilianza Tanzania wakati ukoloni ulipoingia hasa kuanzia miaka ya 1920. Ukoloni unahusu jamii mbili ambapo jamii moja yenye nguvu huitawala jamii nyingine. Katika hali kama hii, hutokea tamaduni mbili – utamaduni unaokandamiza na ule unaokandamizwa. Katika kipindi hiki palikuwepo: Tamthiliya za Kizungu, Vichekesho naTamthiliya ya Kiswahili.
Tamthiliya za Kizungu
Tamthiliya za kizungu zilikusudiwa ama kuwaburudisha maofisa na walowezi (masetla) wa kizungu, au kufundisha Bibilia na imani ya Kikristo.Tamthiliya hizi ziliigizwa kuanzia miaka ya 1920, nyingi zilichezwa mashuleni. Shule ndio hasa zilitumika kuonyeshea tamthiliya zilizojaa ujumi, amali na itikadi ya Kibepari. Kwa sababu tamthiliya inahitaji kusomwa na kukaririwa kabla ya kuonyeshwa kwenye jukwaa, basi usomi ulikuwa kigezo kikubwa cha kufanikisha tamthiliya. Hali hii iliwafanya wala tu waliojua kusoma na kuandika Kiingereza waimudu fani hii. Hawa walipatikana shuleni tu ukiondoa wakoloni wenyewe. St. Joseph Convent School, hivi sasa Forodhani, ilianza kuonyesha tamthiliya za Kiingereza kuanzia 1922. Tamthiliya hizo ni kama vile The Sherrif’s Kitchen, The Ugly Duckling ya Milne na The Birds of a Feather ya Francis. Nyingi katika tamthiliya hizi zilikuwa zile za wakati wa Victoria huko Uingereza (1893-1914). Tamthiliya hizi zilijulikana kama ‘Drawing Room Drama’. Zilijishughulisha na masuala ya kinyumbani, yaani jinsi familia ya Kiingereza huishi, matazamio yake na mambo yafafanayo na hayo. Kwa kifupi, tamthiliya hizi zilitakiwa kuwa na ujumi-taaluma wa tamthiliya, yaani lugha na mtindo wa uonyeshaji uliotakiwa Uingereza wakati huo – ‘Four Wall-Bourgeois Theatre’Tamthiliya zote zilikuwa kwenye Kiingereza. Baadhi ya tamthiliya zilitokana na michezo iliyoandikwa na Waingereza, kwa mfano Shakespeare, na baadhi zilikuwa ni za dini ya
Kikristo.
Takriban tamthiliya zote za kipindi hiki zilikuwa ni za kibwanyenye, yaani zisizopingana na mfumo wa ubepari na ukoloni uliokuwepo. Tamthiliya chache mno zilitafsiriwa kwa Kiswahili, kwa mfano, tamthiliya ya Moliere, ‘Le Medecin Malge Lui’ “Tabibu Asiyependa Utabibu”. Mbali na shule, zilianzishwa taasisi zingine zilizojishughulisha na tamthiliya. Hindu Volunteer Corps ambayo ilionyesha tamthiliya za Kihindi ilianzishwa mnamo 1938. Baadaye, vilianzishwa vikundi vya kuigiza tamthiliya za kizungu: Dar es Salaam players (Little Theatre, 1947) na Arusha Little Theatre, 1953 (Lihamba, 1985:38). Tamthiliya katika lugha ya Kiingereza ilizidi kushamiri baada ya kufanyika mkutano wa wakoloni wa Kiingereza huko Cambridge mwaka wa 1948 uliojulikana kama ‘Cambridge Summer Conference’. Mkutano huu uliongelea suala la kutumia maonyesho kama kipengengele kimoja cha kueneza utamaduni wa Kiingereza kwenye makoloni. Kwa hiyo, matombola, brass bendi na tamthiliya vikatiliwa mkazo. Matokeo ya mkutano huu kwenye makoloni ikawa ni uanzishwaji wa mashindano ya tamthiliya shuleni. Mnamo mwaka wa 1957, Baraza la Kiingereza (British Council) lilianzisha mashindano ya uigizaji wa tamthiliya za Kiingereza nchini Tanzania, yaliyoitwa ‘School Drama
Competition’. Tamthiliya zote zilibidi kuwa kwenye lugha fasaha ya Kiingereza. Mashindano hayo yaliendelea hadi 1963, yalipoanza kusimamiwa na Youth Drama Association. Kuanzia wakati huo, tamthliya za Kiswahili zilianza kuhusishwa katika mashindano hayo, na hivyo kuchochea utuzi wa tamthiliya katika lugha hiyo.
Vichekesho
Vichekesho1 ni aina ya tamthiliya-gezwa (zilizotungwa papo kwa hapo bila kuandikwa). Zilianza miaka ya 1920 kwa lengo la kuburudisha wenyeji. Tamthiliya hizo kwa kawaida zilikuwa na vituko vya kuchekesha na ziliwasuta watu waliofikiriwa kuwa ‘washamba’, ‘wajinga’ au ‘wasiostaarabika’. Tamthiliya hizo zilimwonyesha mhusika anayetoka shamba na kwenda kuzuzuka mjini. Vichekesho viliendelea hata baada ya uhuru (na bado vipo) ila dhamira
zake zilibailika.
Tamthiliya-Andishi ya Kiswahili

 Kipindi cha Uhuru

Tamthiliya ya Kizungu
Tamthiliya ya kizungu iliendelea kuigizwa hata baada ya uhuru, hasa mashuleni na katika kumbi maalumu za maonyesho kama Little Theatres. Hata hivyo, umaarufu wake ulipungua kiasi, hususan upande wa Tanzania. Baadhi ya tamtiliya muhimu za kizungu zilianza kutafsiriwa na kuigizwa kwa lugha ya Kiswahili ili zieleweke zaidi na wananchi km. tafsiri za J.K. Nyerere za Shakespeare, Juliasi Kaisari (OUP, 1964) na Mabepari wa Venisi (OUP, 1969); tafsiri za S.S. Mushi za michezo ya Shakespeare ya Makbeth (TPH, 1968) na Tufani (TPH, 1969); Moliere, Mchuuzi Muungwana (A. Morrison, EALB 1961) na Mnafiki (L. Taguaba, TPH 1973); Sophocles, Mfalme Edipode (S.S. Mushi OUP, 1971); Gogol, Mkaguzi Mkuu wa Serikali (C. Mwakasaka, HEB 1979), nk. Licha ya tamthiliya za kizungu, kadhalika tamthiliya za Kiafrika zilizoandikwa kwa lugha za kigeni na lugha nyingine za kiafrika, zilifasiriwa kwa Kiswahili km. Mtawa Mweusi (Ngugi wa Thiong’o, HEB, 1978); Soyinka W. Masaibu ya Ndugu Jero (Mf. A.S. Yahya OUP 1974); O. Ijimere, Kifungo cha Obatala (HEB, 1978); Ngugi wa Thing’o na Ngugi Mirii, Nitaolewa Nikipenda (HEB, 1982); M. Mulokozi (1968), The Tragedy of Mkwawa (Mf. Kahingi, 1970).

Vichekesho
Baada ya uhuru vichekesho vilichua sura tofauti kidogo. Badala ya kuwasuta ‘washamba’ vilianza kuwasuta ‘wazungu weusi’, yaani waafrika wanaoringia elimu au vyeo na kudharau utamaduni wao (Darlite 2/2: 133-152). Vipengele kama matendo, maonyesho na maongezi vilitumiwa katika uundaji wa vichekesho hivi. Baadhi ya vichekesho, hasa vinavyoonyeshwa kwenye mabaa na sehemu nyingine za burudani na starehe, hujaribu kuzungumzia matatizo ya watu wa kawaida, km. matatizo ya familia, ukosefu wa kazi, ukimwi, uhalifu, udanganyifu wa waganga wa jadi, nk.Vipo pia vichekesho vya kisiasa vyenye kuzungumzia kadhia za kisiasa, ubinafsi wa viongozi, matatizo yanayokumba watu vijijini, mijini, nk. Baadhi ya vichekesho vya redio Tanzania, km. “Mahoka” (kipindi kilichoanza mwaka 1974) na “Pwagu na Pwaguzi” (kilianza mwaka 1978), hukejeli na kukemea tabia mbovu za baadhi ya watu, wakiwemo viongozi wa kiasa. Siku hizi vichekesho hutangazwa na vituo vya redio na televisheni, na huonyeshwa mijini kwenye kumbi za starehe.
 Tamthiliya-Andishi ya Kiswahili
Baada ya uhuru utunzi wa tamthiliya ulipamba moto zaidi, hasa upande wa Tanzania. Uhuru uliwafanya waandishi wa tamthiliya kuandika mambo ambayo wasingeweza kuyaandika hapo awali. Waandishi walitumia tamthiliya kuelezea matatizo yanayokabili jamii. Mashindano ya utunzi na uigizaji yaliyoendeshwa na Youth Drama Association nchini Tanzania yaliwawezesha watunzi chipukizi kujitokeza, akiwemo Ebrahim Hussein ambaye tamthiliya yake ya kwanza, Wakati Ukuta (EAPH,1969) ilishinda tuzo katika mashindano hayo. Wengine walikuwa Uhinga na Katalambula ambao walitunga tamthiliya za Kiswahili zilizoonyesha maadili katika jamii. Wakati huo pia ndipo walipoanza kutokea watunzi waliohitimu fani ya sanaa za maonyesho katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam km. E. Hussein, P. Muhando, N. Ngahyoma na G. Uhinga. Kwa mujibu wa Mulama (1983) watunzi walianza kuifungamanisha tamthiya na mahitaji ya nchi ya Tanzania. Uzukaji wa tamthiliya ukaambatana na hali maalumu za kiuchumi na kijamii.

MAREJELEO.

No comments:

Post a Comment

hakiki na tuma maoni au mapendekezo kuhusu makala hii ya andiko langu la uchunguandiko langu

ANDIKO LA UCHUNGU (Kwa shemeji zangu na wanangu)           NYAMBUYA OGUCHU,                            S.L.P 777666,       ...