Thursday, July 14, 2016

Tanzia ramsa ya ni tanzia inayoishia kwa furaha, vipi kauli hii inaaksi tamthiliya ya Orodha ya Steve Reynolds kwa mujibu wa nadharia ya uhalisia?



Tanzia ramsa ya ni tanzia inayoishia kwa furaha, vipi kauli hii inaaksi tamthiliya ya Orodha ya Steve Reynolds kwa mujibu wa nadharia ya uhalisia?
Maana ya tanzia ramsa
Wamitila (2003:219) anaeleza tanzia ramsa kama aina ya tanzia ambayo inahusisha mbinu za futuhi aghalabu kwa kuishia kwa furaha. Hali hii inaweza kupatikana kwa kuwepo kwa hasidi au muwi anayetubu na kuyajutia makosa au msimamo wake au kuwepo kwa mandhari ya kiulimbwende. Anaendelea kufafanua kuwa tanzia ramsa huweza kutumiwa pia kwa tanzia ambayo ina kisuko cha kuchekesha ambacho kinakuwa kama kijalizo cha msuko mkuu wa kitanzia.
Kutokana na maana hiyo, tunaweza kufafanua tanzia ramsa kuwa ni mchezo wa kuigiza wenye visa au matukio mazito ya kitanzia ambayo kadri ya mchezo unavyoendelea matukio hayo hugeuka ghafla na kuwa ya furaha. Mara nyingi mgeuko huo wa matukio hutokea kipindi ambacho wahusika wake wapo katika kipindi cha kuendewa na mambo vibaya na hatimaye kugeuka na mambo kuenda vizuri, na huwa ni mwishoni mwa mchezo.
Sifa za tanzia ramsa
Tanzia ramsa ina sifa zake ambazo huitofautisha na aina zingine za tamthilia. Baadhi ya sifa hizo ni kama zifuatazo:
  1. Hukejeli ujinga wa binadamu na kuonesha udanganyifu au uovu alionao binadamu.
  2. Matukio katika tanzia ramsa hugeuka gafla kutoka katika hali ya kitanzia kwenda katika hali ya furaha na ugeukaji huu wa matukio haubashiriki. Kwa mfano, katika tamthlia ya Orodha.
  3. Uongo mwingi hutumika, yaani wahusika wake wengi huchorwa na mwandishi kuwa na tabia ya uongo. Kwa mfano Padri James katika tanzia ramsa ya Orodha.
  4. Hadhira haiwaonei huruma wahusika wakuu kutokana na matendo yao maovu wanayofanya bali hukejeliwa na kuchekwa.
  5. Wahusika wakuu huonekana kuendewa na mambo vizuri ingawa hukumbwa na matatizo mengi.
  6. Aghalabu tanzia ramsa huishia kwa furaha.
  7. Wahusika wakuu hufanya harakati mbalimbali za kijikomboa kutokana na tatizo linalowakumba ili kuficha maovu yao, yaani wasionekane waovu kwa jamii yao. Kwa mfano Bwana Ecko katika tamthilia ya Orodha ambaye alijitihadi kwa hali na mali kuitafuta orodha ili asionekane muovu mbele ya mkewe na jamii kwa ujumla, lakini pia padri James, Salim na Juma wanadhihirisha harakati hizo.
Maana ya nadharia ya uhalisia
Malenya, (2012:197) anafafanua kuwa uhalisia unatumika kama njia ya kutathimini hali ya uhalisia wa maisha kiuyakinifu au uhakika wa maisha. Uhalisia unahusu uigaji wa maisha anapopatikana mwandamu. Mwanafalsafa Hegel katika kitabu chake cha Aesthetics alitumia neno uhalisia kumaanisha kazi ya saana iliyo na wahusika ambao matendo yao yanayochochewa na hali ya kisaikolojia iliyowazunguka. Waandishi huzungumzia, huchambua, na kuchagua mambo anayotaka kuyasema huku akisuta maovu katika jamii.
Wafula na Njogu (2007:62) katika kitabu chao cha Nadharia za Uhakiki wa Fasihi wanadai kuwa, uhalisia wa kifasihi unaashiria uwezo wa kusawiri au kuelezea hali kwa kuzingatia uyakinifu au uhakika wa maisha. Vilevile wanaendelea kusema kwamba, uhalisia unahusu uigaji wa mazingira anamopatikana mwanadamu.
Wamitila (2003:272) anafafanua kuwa uhalisia ni mkondo unaosisitiza usawiri wa matukio au maisha katika fasihi kama yalivyo katika maisha ya kila siku. Mmoja kati ya wataalamu wanaohusishwa na dhana hii ni mfuasi wa Marx kutoka Hungary aliyejulikana kama George Lucas ambaye aliamini mambo kadha wa kadha kama vile usawiri wa uhalisia katika ukamilifu wake, kuchunguza undani wa picha inayoonekana ya uhalisia na kugundua sheria za mabadiliko ya kihistoria zinazosababisha hali fulani.
Pia tumkimfasili Senkoro (1987) akirejelea maelezo ya Engles juu ya dhana ya uhalisia anadokeza zaidi na kueleza jambo katika undani na ukweli wake na usawilishaji wa kiukweli wa wahusika katika mazingira yao na matendo yao.
Kwa hiyo, isitilahi uhalisia katika taaluma ya falsafa ilimanisha uhalisia au ukweli wa mawazo dhidi ya falsafa zilizochukuliwa za majitu au dhana tu za kidhahania. Kwa upande wa fasihi na sanaa istilahi uhalisia ilikita mizizi enzi za utawala wa Malkia Victoria wa Uingereza na mapinduzi ya viwanda. Katika nadharia hii maisha yanaelezwa kama yalivyo katika uhalisia wake.
Kwa ujumla nadharia hii imejikita katika mawazo makuu yafuatayo kama yalivyojadiliwa na wataalam mbalimbali wakiwemo Malenya (2012) na Wafula na Njogu (2007):
  • Wanauhalisia hutambua maisha yanayomzunguka binadamu kama chanzo cha ubunifu.
  • Uzingativu wa hali ya juu wa maisha jinsi yalivyo.
  • Jukumu la kazi yoyote ya fasihi (sanaa) ni kuelimisha na kufunza jamii.
  • Wahusika wa kiuhalisia husawiriwa kwa kazi zao za kila siku ili kuonesha uhalisia wa shughuli zao.
  • Tukio la kiuhalisia hutumika huku likitafutiwa sheria za kisayansi ambazo zilisababisha tukio hilo kutokea.
Jinsi ambavyo tanzia ramsa huishia kwa furaha kwa kuzingatia nadharia ya uhalisia.
Tanzia ramsa ni tanzia ambayo kwa kawaida huishia kwa furaha kutokana na mgeuko wa ghafla wa matukio, kwa kuzingatia nadharia ya uhalisia, ufuatao ni ushahidi unaothibitisha kauli hii kwa kurejelea tamthilia ya Orodha ya S.Reynolds:
Tamthiliya ya Orodha ni tanzia ramsa ambayo mtiririko wa hadithi unaanza kujengeka katika tukio la baba Furaha na mama Furaha kujadiliana juu ya malezi na mwenendo wa binti yao Furaha (uk.5). Hali hii inaaksi maisha ndani ya jamii ambapo inaonekana wazazi hukaa na kujadili kuhusiana na mienendo ya watoto wao pale wanapoonekana kutoenenda vyema, lengo kuu likiwa ni kutaka kuwajenga katika njia bora za kuishi katika jamii. Hali hii inasawiri mawazo ya wanauhalisia pale wanaposema kuwa jukumu la kazi yoyote ya fasihi ni kuelimisha na kufunza jamii.
Ni usiku, furaha akiwa amelala na wadogo zake chumbani, sauti ya Mary inasikika dirishani ikimuita Furaha ili waende baa kukutana na akina Bw. Ecko na Juma waliokuwa wakiwasubiria. Wakiwa baa Bw. Ecko anaanza kumtongoza Furaha kwa kumsifia uzuri wake pamoja na kumpa pombe iliyomsababisha kulewa na hatimaye kwenda kulala naye. Kitendo hiki kinasadifu maisha ndani ya jamii kwani vijana wengi huonekana kuingia katika matendo yasiyofaa kutokana na ushawishi wa marafiki na tamaa zisizofaa, hali ambayo huwapelekea kuishia katika matatizo kama vile maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU). Hali hii inasawiri wazo la wanauhalisia linalojikita katika uzingativu wa hali ya juu ya maisha jinsi yalivyo.
Baaada ya Furaha kutembea na Bw. Ecko anaamua kwenda kutubu kwa Padri James. Kutokana na uzuri wa Furaha Padri James anajawa na ushawishi wa kimapenzi dhidi ya binti huyu mrembo. Na siku iliyofuata wakiwa katika chumba cha maombezi, Padri James na Furaha wanaingia katika dimbwi la mahaba na hatimaye kuzini. Kitendo hiki kinasadifu hali halisi ndani ya jamii zetu kwani watu wanapofanya maovu hutafuta njia ya kujitakasa mfano kwenda kanisani kutubu. Lakini pia katika jamii kuna viongozi wa dini ambao si waaminifu kwani hujikuta wakiangukia katika vitendo visivyofaa na waumini wao kwa kisingizio cha kwamba wao nao ni binadamu. Mfano Padri James anasema…Kuna shinikizo kubwa, vishawishi vingi! kwa watu hawa, mimi ndiye Padri wao… lakini mimi pia ni mwanadamu! Mahitaji yote haya ni ya mwanadamu. Hali hii pia inadhihirisha wazo la wanauhalisia kwamba wahusika wa kiuhalisia husawiriwa kwa kazi zao za kila siku ili kuonesha uhalisia wa shughuli zao, mfano Padri James.
Siku moja Furaha akiwa njiani kuelekea sokoni anakutana na Kitunda akiwa na sterio yake begani. Kitunda anaanza kumtongoza kwa kumsifu na kujinadi yeye mwenyewe kupitia sterio yake na uzuri wa mji wa Dar es Salaam. Mfano mazungumzo ya Kitunda na Furaha (uk.13) “Kitunda: Unakwenda wapi; mshikaji?
Furaha: Nimetumwa sokoni na mama.
Kitunda: Wewe, mtoto bomba kichizi. Hee, kwanini hupumziki kidogo na kufaidi
midundo?
Furaha: Siwezi, nitachelewa nyumbani.
Kitunda: Aaa mshikaji, mi sikwambii uwe binti mbaya. Kaa kidogo tu. Yaani
kama hilo unaliona noma. Unaogopa, sivyo?
Furaha: Siogopi…
Kitunda: Hii nimeipata kutoka Dar es Salaam, mshikaji!
Furaha: Dar! Napenda sana nami siku moja nifike huko!
Kitunda: Ni bomu, mshikaji wangu...
Furaha: (Akija karibu zaidi – sasa amevutiwa) Eenh! Na umefika huko?
Kitunda: (Anamtania) Kisura, ni kama jiji la New York ya Afrika Mashariki!
Nakwambia, mwanangu, kule kuna majengo makubwa kiasi…”
Kitushi hiki kinasadifu maisha halisi ndani ya jamii zetu ambapo vijana wa kiume hutumia maneno ya kuwavutia mabinti ili waweze kuwashawishi na hatimaye kutimiza malengo yao ya kuwaingiza katika vitendo vya ngono zembe, hali ambayo hupelekea athari mbalimbali za kiafya kwa vijana hao. Hali hii inadhihirisha wazo la wanauhalisia la uzingatiaji wa maisha ya binadamu jinsi yalivyo.
Salim (mchumba wake Furaha) anarudi kutoka masomoni Dar es Salaam na kukutana na mchumba wake baaada ya kipindi cha miaka miwili. Salim anaamua kumuuliza Furaha kama kaweza kumsubiri kwa muda ambao yeye alikuwa masomoni. Furaha anamjibu kwa kumtoa hofu kuwa kamsubiri na asiwe na hofu juu yake; japo kiukweli Furaha kashavunja ahadi kwa kutembea na wanaume wengine kijijini. Baada ya mazungumzo yao wanaamua kukutana usiku nyuma ya nyumba bila ya Furaha kumueleza ukweli mchumba wake juu ya yale aliyoyatenda na akina Bw. Ecko, Padri James na Kitunda. Mfano mazungumzo ya Furaha na Salim (uk.16-17). Kupitia hali hii ya kutokuwa na uaminifu kati ya Furaha na Salimu wazo la wanauhalisia la kwamba jukumu la kazi yoyote ya fasihi (sanaa) ni kuelimisha na kufunza jamii linadhihirika kwani elimu inapatikana kupitia hali iliyomfika Furaha na Salim.
Wanakijiji wanazungumzia kuhusu tabia ya furaha, wanasema kuwa Furaha amekuwa kama punda kila mtu anampanda pale kijijini. Wakiwa katika mazungumzo hayo, mama Furaha anawakuta na wanaamua kutawanyika isipokuwa mwanakijiji wa tatu ambaye anabaki na mama Furaha. Mwanakijiji huyo anamueleza mama Furaha kuhusu tabia za Furaha. Baada ya mama Furaha kurudi nyumbani alitaka kuyathibitisha kwa mtoto wake yale aliyoyasikia kwa mwanakijiji, lakini Furaha alikataa katakata. Dalili za kuugua Furaha zinaanza kuonekana baada ya kuanza kukohoa mfululizo, kuishiwa nguvu na kupungua uzito. Baada ya kupimwa, vipimo vinathibitisha kuwa Furaha ana VVU/UKIMWI. Katika jamii yetu ya sasa kuna akina Furaha wengi ambao wao wanapoulizwa na kuonywa kuhusu tabia mbaya wao hawataki kusema ukweli wala kusikiliza mwishowe kuishia katika matatizo kama ya Furaha. Hali hii husawiri wazo la wanaualisia ambalo ni uzingativu wa hali ya juu ya maisha jinsi yalivyo.
Habari za ugonjwa wa Furaha zinaenea kijijini pale ambapo wanakijiji wanazungumza kuhusu ugonjwa wake huku wakiwa hawajui ni ugonjwa gani na kaupataje. Wengine wanasema unaambukizwa kwa kugusana (uk 25-26), wengine wanasema hata kwa kuwa na mgonjwa katika chumba kimoja. Pia habari zinaenea kuwa Furaha ameandika barua ambayo ina orodha ya majina ya wanaume waliotembea naye, kitu knaichomfanya Salim kwenda kwa Furaha ili kujua ukweli huo na ikiwezekana aione hiyo barua lakini Furaha anakataa kumpatia. Salim anafukuzwa na Mama Furaha bila kufanikiwa kuiona ile barua. Baada ya pale Furaha anakata roho mikononi mwa mama yake baada ya kuugua kwa muda mrefu. Baada ya kifo cha Furaha, Bw. Ecko, Juma na Kitunda wanaingiwa na wasiwasi kuhusu ile orodha iliyoachwa na Furaha huenda ikawa na majina yao. Hali hii inasadifu uhalisia katika jamii yetu kwani watu wengi wamekuwa wakieneza taarifa za wagonjwa hasa kwa wale ambao wanakuwa na gonjwa la UKIMWI bila hata kuwa na uelewa wa nini chanzo cha ugonjwa huo. Imani za kishirikina pia zimekuwa zikihusishwa na ugonjwa huo. Kitushi hiki kinasawiri wazo la wanauhalisia kuwa tukio la kiuhalisia hujadiliwa huku likitafutiwa sheria za kisayansi.
Baada ya kupata taarifa hizo za Orodha iliyoandikwa na Furaha, Bw. Ecko, Kitunda na Padri James nao wanaanza harakati za kuisaka ili kujiepusha na aibu katika kijiji chao. Bw. Ecko na Juma wanaingia kwenye chumba chenye maiti ya Furaha na kuanza kutafuta ile barua, wanakutwa na baba Furaha lakini wanajificha kwenye jeneza lenye maiti. Baadaye Kitunda anaingia na wote watatu wanaisaka ile barua bila mafanikio na hatimaye kukimbia baada ya kukutwa kwa mara nyingine tena. Siku ya mazishi Padri James naye anajitahidi kuisaka orodha sehemu mbalimbali ndani kwa akina Furaha baada ya kuomba aachwe peke yake ili akusanye mawazo matakatifu. Padri James anatafuta barua kabatini, kwenye makochi, hadi kwenye chungu kidogo ambacho kinang`ang`ania mkononi mwake bila kufanikiwa kuipata barua, na anapokutwa anadai anatafuta rozali ilihali ipo shingoni mwake. Vivyo hivyo watu katika jamii zetu hutafuta mbinu mbalimbali za kutatua tatizo ili kuficha aibu baada ya kufanya mambo yasiyokubalika katika jamii. Hali hii inasawiri wazo la wanaualisia kuwa, wanaualisia hutambua maisha yanayomzuka binadamu kama chanzo cha ubunifu.
Tamthiliya hii inaishia kwa mazishi ya Furaha ambapo siku hiyo asubuhi akina Bw.Ecko, Juma na Kitunda wanaonekana wakiwa baa wakisimuliana msako wa barua siku iliyopita. Pia wakiwa mazishini wanaonekana wakiwa na wasiwasi wa majina yao kusomwa kwani bado hawajafanikiwa kuipata ile orodha. Mama Furaha anapojiandaa kusoma ile barua, Salim anaikwapua na kuichanachana. Baada ya hapo akina Bw. Ecko, Juma, Kitunda na Salim wanajawa na furaha na hata Padri James kwani yeye mwenyewe ndiye mmoja wa wahusika hao waliokuwa wakiisaka ile orodha. Hii inadhihirisha ukamilifu wa tanzia ramsa kuishia kwa furaha. Isitoshe hata baada ya vile vipande kuokotwa na ujumbe ulioachwa na Furaha kusomwa wanakijiji wanajawa na furaha kwani wamepata elimu kuhusu gonjwa la UKIMWI. Ujumbe huo ni orodha ya mambo kumi ambayo yanaweza kumsababishia mtu kupata au kuepuka maambukizi ya VVU/UKIMWI, mambo hayo ni kondomu, uaminifu, uelewa, elimu, uwazi, uadilifu, uwajibikaji, ukweli, upendo, na msamaha. Kupitia orodha hii wazo la wanauhalisia linadhihirika kwamba jukumu la kazi yoyote ya fasihi (Sanaa) ni kuelimisha na kufunza jamii.
Hivyo tunaweza kuhitimsha kuwa tamthiliya ya Orodha imejikita zaidi katika uhalisia ambao umejitokeza kupitia wahusika waliotumika, kwni wapo walioamini ushirikina kama mama Furaha, usaliti katika mapenzi kama vile Bw.Ecko, Salim, na Furaha, na ukahaba ambao katika jamii umeshamiri hasa maeneo ya mjini. Pia katika jamii yetu kuna watu kama akina Juma, Padri James na Salim ambao hawapendi ukweli na uwazi. Fauka ya hayo, ukosefu wa adabu kwa vijana, kuziba masikio na kutopokea ushauri wa wazazi, ulevi na matumizi ya madawa ni tatizo lingine linalowakumba vijana kwa mfano Kitunda katika tamthiliya hii. Hivyo basi, ufahamu wa mambo haya mwishoni mwa tanzia ramsa hukamilisha sifa yake ya kuishia kwa furaha ikiwa ni sifa muhimu ya kuitofautisha tanzia ramsa na tamthiliya zingine.




MAREJEO.
Malenya, M.M. (2012). Matumizi ya Lugha Katika Fasihi Simulizi. Mwanza: Inland
Press.
Reynolds, S. (2006). Orodha. Dar es Salaam: Macmillan Aidan Ltd.
Senkoro, F.E.M.K. (1987). Fasihi na Jamii. Dar es Salaam: Press and Publicity Centre.
Wafula, R. M. & Njogu, K. (2007). Nadharia za Uhakiki wa Fasihi. Nairobi: The Jomo
Kenyata Foundation.
Wamitila, K.W. (2003). Kamusi ya Fasihi, Istilahi na Nadharia. Nairobi: English press.
Focus Publications Ltd.




Tuesday, July 5, 2016

Ulinganishaji wa kitabu cha 'natala' na kile cha 'siku njema'


Maana ya riwaya
Wamitila (2003) anafafanua riwaya kuwa ni kazi ya fasihi andishi ambayo kwa kawaida ni ndefu kuliko hadithi fupi. Urefu wa riwaya maana yake ni kwamba msuko wa simulizi umejengeka vizuri, kuna wahusika wengi, unaenea muda mrefu, na mada zake ni nzito na pana kiasi.
Muhando na Balisidya (1976) wanaeleza kuwa riwaya ni kazi ya kubuni kama hadithi ambayo hutungwa na kuibua mambo mengi katika mazingira wanayoishi watu.
Maana ya Tamthiliya
Tamthiliya ni utanzu ambao hutegemea mazungumzo na uigizaji ili kuwasilisha ujumbe wake. Huu ni utanzu ambao huandikwa kwa mtindo wa mazungumzo ya wahusika, (Wamitila, 2007).
Tamthiliya ni mchezo wa kuigiza au utungo wa kisanaa ambao huweka wazo fulani katika matendo na mazungumzo
Muhtasari wa Riwaya ya “Siku Njema.”
Siku njema ni riwaya ya kitawasifu inazungumzia maisha ya Msifuni Kombo (Kongowe Mswahili) iliyoandikwa na mwandishi Ken Walibora mnamo mwaka 1996. Riwaya hii imejikita katika kuzungumzia mambo yanayoendelea katika jamii zetu za Kiswahili kama vile changamoto za magonjwa, ndoa na familiya pamoja na malezi ya watoto. Mwandishi kamtumia mhusika mkuu Msifuni Kombo maarufu kama Kongowea Msawahili kuonesha namna alivyopitia changamoto mbalimbali zikiwemo kufiwa na mama yake, kulelewa na mzazi mmoja (mama yake) baada ya mama kumkataa baba yake Kongowea aliyejulikana kwa jina la Juma Mukosi. Kongowea anapitia mateso mengi hata kutiliwa sumu kwenye chai na mkaza-mjomba (Mwanasaumu) ili afe.
Wasifu wa Prof. Ken Walibora
Ken Walibora alizaliwa Magharibi mwa Kenya na alisoma elimu ya msingi katika shule ya St. Joseph iliyoko wa mji wa Kitale. Alihitimu elimu ya kidato cha nne katika shule ya upili ya Olkejuado, mjini Kajiado. Na alihitimu mtihani wa kidato cha sita katika shule ya upili ya Koelel, mjini Gilgil. Walibora baadae alisomea masuala ya Maendeleo ya Jamii katika Taasisi ya Utawala, Kenya (KIA). Alihitimu shahada ya kwanza katika fasihi na Kiswahili katika chuo kikuu cha Nairobi. Prof. Walibora ni msomi mwenye PhD aliyoipatia nchini Kenya katika Chuo kikuu cha Ohio State nchini Amerika. Riwaya yake ya kwanza kuandika ni “Siku Njema” iliyochapishwa mwaka 1996 na amekwisha andika zaidi ya vitabu arobaini baada ya riwaya hiyo.
Ufafanuzi wa vipengele vya ulinganishaji katika riwaya ya “Siku njema”
Vipengele tulivyochunguza ni plot (muundo), mandhari, wahusika na migogoro. Vipengele hivyo vimefafanuliwa kwa kina kama ifuatavyo:
Ploti (muundo); ni namna matukio katika kazi ya fasihi yalivyopangwa na kuleta mtiririko wa kazi husika ya fasihi (Senkoro, 2011). Katika riwaya ya “Siku njema” iliyoandikwa na Ken Walibora, mwandishi amejenga visa na matukio katika mtiririko unaoeleweka kwa urahisi kwa msomaji. Kwa hiyo ni dhahiri kusema kuwa mwandishi wa riwaya hii ametumia muundo wa msago (muundo wa moja kwa moja) ambapo ameonesha mtiririko ufuatao:
Katika sura ya kwanza; ameonesha historia na asili ya Zainabu Makame ambayo imejengeka kupitia familiya ya Mzee Makame iliyoishi mjini Mwanza kabla ya mzee Makame kufariki.
Sura ya pili; Bibi yake Kongowea amerudi Tanga na Zainabu anajiunga na kikundi cha Mbelewele taarabu na kupata umaarufu kutokana na sauti yake nzuri katika uimbaji.
Katika sura hii pia kuzaliwa kwa Msifuni Kombo (Kongowea mswahili) kunadhihirika. Pia katika sura hii inaonesha Zainabu Makame anaanza kuugua.
Sura ya tatu; mwandishi anaonesha Zainabu akiaga dunia baada ya kuugua muda mrefu na kukosa tiba ya maradhi yaliyomsumbua. Lakini mama huyu anafariki bila kumuonesha mwanae baba yake.
Sura ya nne na kuendelea inadokeza changamoto alizopitia Kongowea hasa baada ya kwenda kuishi kwa mkaza-mjomba wake (Mwanasaumu).
Katika sura ya tano na kuendelea mwandishi ameonesha harakati za Kongowea kumtafuta baba yake na hatimaye anafanikiwa kukutana naye kama mwandishi anavyoonesha kuanzia mwishoni mwa sura ya kumi na tatu mpaka kumi na nne.
Baada ya Kongowea kukutana na baba yake aliyejulikana kwa jina la Juma Mukosi, baba huyo anafariki kabla ya mwanaye kumtambua na kuacha wosia unaomuongoza mwanae kutambua mali alizotakiwa kuzirithi kutoka kwa baba yake. Baada ya kuupata wosia ule maisha ya Kongowea yanabadilika baada ya mahangaiko ya muda mrefu tangu kuzaliwa kwake.
Mandhari; huwa ni mahali hususani jinsi panavyoonekana katika hali halisi ya maisha (Williady, 2015). Mtunzi anaweza kutumia mandhari kuelezea mazingira halisi ya kisa anachosimulia. Pia mtunzi huweza kusawili mazingira mbalimbali akiyasawiri matukio tofautitofauti ikiwa ni mbinu mojawapo ya kufikisha ujumbe wake kwa jamii husika. Hivyo mandhari humsaidia msomaji kung’amua ujumbe akirejelea tukio husika.
Mwandishi Ken Walibora katika riwaya hii ameweza kujenga visa na matukio katika mazingira halisi (mandhari halisi). Mandhari aliyotumia imejumuisha maeneo ya nchi mbili za Afrika ya Mashariki ambazo ni Tanzania akirejelea maeneno ya Mwanza- huku ndipo alipozaliwa Zainabu Makame mnamo mwaka 1927 (uk.15), Chongoleani- mkoani Tanga ambako walizaliwa babu na bibi zake Zainabu (uk.2), Tabora-mahali pa makazi ya Enock Minja mpwa wa Mwanasaumu (uk.23), Hospitalini (Holelaholela) ni pale alipopelekwa Bi. Rahma kwa ajili ya matibabu (uk.28), Arusha ni sehemu Vumilia alikuwa anasoma (uk. 45), Buguruni-Dar es Salaam-mahali alipokuwa anafanya kazi mama yake Alicia (uk.109). Nchini Kenya mwandishi amerejelea maeneo ya Mombasa- mahali alipokuwa anakaa Salimu ambaye ni mjomba wake Kongowea (uk.18), pia ni sehemu ambapo Enock Minja alifikwa na mauti baada ya kupata ajali ya gari, vilevile ndiko alikohamia baba yake Kongowea katika ule mji wa Kitale (uk.33).
Wahusika; ni viumbe hai au viumbe visivyo hai ambavyo hubebeshwa majukumu na msanii ili kuifikishia hadhira ujumbe uliokusudiwa na mwandishi (Williady, 2015). Mwandishi Ken Walibora katika riwaya ya “Siku Njema” amadhihirisha wahusika ambao tunaweza kuwaweka katika makundi matatu kutokana na hadhi ya uhusika wao, makundi hayo ni wahusika wakuu, wahusika wasaidizi na wahusika wajenzi kama yalivyofafanuliwa hapa chini:
  • Mhusika mkuu; katika riwaya hii mhusika mkuu ni Msifuni Kombo maarufu kwa jina la Kongowea Mswahili kwani ndiye aliyebeba dhamira kuu ambayo ni familia na malezi akiwa kama mtoto aliyekosa malezi ya baba na kulelewa na mama, lakini mama yake naye anafariki na kulelew na mjomba. Pia mhusika huyu ndiye alidhihirisha mantiki ya tawasifu katika riwaya hii kwani mtiririko wake unadokeza historia yake toka kuzaliwa mpaka kufiwa na wazazi wote wawili.
  • Wahusika wajenzi; hawa huwa ni wahusika wanaoibuliwa na mwandishi ili kujenga dhamira na baadae hutoweka. Katika riwaya hii wahusika wajenzi ni pamoja na Bi. Mack Donald ambaye ameibua dhamira ya upendo baada ya kumsaidia Kongowea katika mkahawa; Enock Minja ambaye ameibua dhamira ya dhuluma ya urithi na tamaa ya mali baada ya kukubali kujifanya mtoto wa Juma Mukosi ili akarithi mali na matokeo yake anafariki kwa ajali ya gari kabla hajafika kwa Juma Mukosi.
  • Wahusika wasaidizi; hawa ni wahusika ambao humsaidia mhusika mkuu katika ujengaji wa dhamira. Kwa mfano Ken Walibora amemtumia Bi. Zainabu Makame kama mama yake Kongowea Mswahili ili kuibua dhamira ya malezi ya watoto; Kitwana ametumiwa kama mjomba wake Kongowea anayemchukua na kuishi naye baada ya kufiwa na mama yake. Alikuwa mshauri mkuu wa Kongowea; Vumilia pia ni mhusika aliyeshiriki kama msaidizi kwani alichorwa kama rafiki yake Kongowea na baadaye akaja kuwa mke wake. Huyu ndiye aliyemdokeza Kongowea kuwa kuna mpango wa kutiliwa sumu kwenye ili afe uliopangwa na mkaza-mjomba wake.
Mgogoro; ni hali ya kutoelewana baina ya pande mbili yaani mtu na mtu, mtu na kundi, mtu mwenyewe na nafsi yake. Mgogoro ni mivutano na misuguano mbalimbali katika kazi ya fasihi. Migogoro inaweza kuwa kati ya wahusika na familia zao, au matabaka yao. Pia migogoro inaweza kugawanyika katika vipengele vikuu viwili ambavyo ni mgogoro wa nafsia na mgogoro wa mtu na mtu au kundi kama ilivyodhihirishwa na Ken Walibora katika riwaya ya “Siku Njema”.
  • Mgogoro wa Nafsia; ni aina ya mgogoro unaotokea baina ya mtu na akili au nafsi yake mwenyewe pale anapojikuta katika wakati mgumu kutokana na jambo fulani na asijue nini cha kufanya.
Mgogoro huu umedhihirika kwa Kongowea baada ya kifo cha mama yake akibaki hajui ni namna gani atampata baba yake. Suluhisho la mgogoro huu pale alipoambiwa na Bi. Rahma baba yake aliko;
pia mgogoro wa aina hii unadhihirika kwa Juma Mukosi maarufu kwa jina la Kazikwisha baada ya kukataliwa na Zainabu hali hii ilimpelekea kuacha kazi. Suluhisho la mgogoro huu ni yeye kuamua kuishi maisha ya ukiwa mpaka siku yake ya mwisho (uk.132)… Baada ya zawadi kunikata maisha yalikosa maana na kazumu kuishi maisha ya ukiwa mpaka siku yangu ya mauko. Nikaacha kazi na kughunia huku makutano kwa ngozi baada ya kununua shamba hili…. Kuishi ukiwa ndiko kumekuwa faraja yangu.
  • Migogoro kati ya mtu na mtu; ni migogoro inayotokea baina ya mtu na mtu au mtu na kikundi au hata familia. Migogoro ya aina hii imejitokeza kati ya wahusika wafuatao;
Mwanasaumu na Kongowea (uk.20-25)
Chanzo cha mgogoro baina ya wahusika hawa ni kufaulu kwa Kongowea katika mtihani wa darasa la saba huku watoto wa Mwanasaumu wakiwa hawajiwezi kimasomo, hivyo hakupenda Kongowea afaulu hali iliyopeleka chuki mpaka akamtilia sumu kwenye chai ili afe. Suluhisho la mgogoro huu ilikuwa Kongowea kuondoka kwa Mkaza-mjomba na kwenda kumtafuta baba yake Kenya.
Kongowea na Selemani Mapunda (uk.21)
Chanzo cha mgogoro huu ni baada ya Selemani Mapunda kubaini kuwa Kongowea ndiye aliyepeleka taarifa polisi kuwa Selemani na wenzake aliwashuhudia wakimpiga Hedimasta. Suluhisho la mgogoro huu ni Selemani Mapunda na Bakari kuuawa (uk.131).
Alice na mama yake (Bi. Mack Donald)
Chanzo cha mgogogoro huu ni mama Alicia kumsaidia Kongowea Mswahili baada ya kumkuta mgonjwa katika mkahawa ulioitwa Saidia Khala, Alice alikasirishwa na kitendo hicho cha mama yake. Alice anasema “…mama huyu mtu unampeleka wapi, akamuuliza bintiye. ‘Shut up’ alifoka mama mtu” (uk.107). Suluhisho la mgogoro huu ni pale tu Alicia anapokuja kutambua kuwa Kongowea ni mahiri wa mashairi na kujikuta wanakuwa marafiki.
Muhtasari wa Tamthiliya ya “Natala”
Tamthilia ya “Natala” ni tamthiliya iliyoandikwa na Profesa Kithaka Wa Mberia mwaka 1997 ambayo imemulika baadhi ya masuala ya kijamii yanayoleta mabishano makubwa. Baadhi ya masuala hayo ni pamoja na kuoza kwa mfumo wa uadilifu na utamaduni unaozivuta jamii nyuma kama vile kurithi wajane na ukatili kwa wanawake (udhalilishaji wa kijinsia) ambao msanii kauchora kupitia mhudumu wa jengo la ufuo kumtaka Natala kimapenzi kwa nguvu wakati amefuata mwili wa marehemu mumewe baada ya kudhaniwa kuwa amefariki kwa ajali ya gari.


Wasifu wa Prof. Kithaka Wa Mberia
Kithaka Wa Mberia alizaliwa mwaka 1955 nchini Keya. Ni mshairi mbunifu wa mashairi huru (mashairi ya kisasa). Amewahi kuchapisha vitabu vinne vya ushairi ambavyo ni Mchezo wa Karata (1997), Bara Jingine (2001), Redio na Mwezi (2005) na Msimu wa Tisa (2007). Maashairi yake yamekuwa mashairi ya kwanza ya Kiswahili kuigizwa katika tamsha la maonesho la kitaifa nchini Kenya mwaka 1988. Wa Mberia pia ni mtaaluma na mwandishi wa tamthiliya. Ni prof. wa lugha katika chuo kikuu cha Nairobi. Ameandika tamthiliya tatu ambapo mojawapo imefanikiwa kurushwa katika runinga nchini Kenya.
Ufafanuzi wa vipengele vya ulinganishaji katika tamthiliya ya “Natala”
Ploti (muundo); kama tulivyoona katika maelezo ya awali, ploti ni namna matukio katika kazi ya fasihi yalivyopangwa na kuleta mtirirko wa kazi husika ya fasihi. Ni jinsi mwandishi alivyoipanga kazi yake (Senkoro, 2011). Mwandishi wa tamthiliya hii amejenga matukio yake katika mtiririko wa matukio kufuatana (muundo wa moja kwa moja) kama inavyodhihirika katika muhtasari ufuatao kuanzia onesho la kwanza hadi la mwisho (la tano):
Onyesho la Kwanza; linadokeza nyumbani kwa Natala akiendelea na shughuli zake. Baadaye Tila anaingia kuomba chumvi, na baadaye kuzua tafrani akidai chumvi aliyopewa ni kidogo.
Onyesho la Pili; linadokeza Chifu akileta taarifa za kufariki kwa Tango nyumbani kwa Natala. Vilevile mwandishi anaonesha Natala na Bala wakiigiza mambo yale waliyokumbana nayo kule kwenye jengo la ufuo baada ya kufuata mwili wa marehemu mochwari (jingo la ufuo).
Onyesho la tatu; mwandishi anaonesha mazishi ya Tango na vikwazo wanavyopambana navyo ndugu wa marehemukutoka kwa chifu ikiwa ni pamoja na kuomba rushwa ili wapate kibari cha kukusanyika kwa ajili ya maziko.
Onyesho la nne; linamuonesha Mama Lime akiwa anamshawishi Natala akubali kuolewa na Wakene lakini anakataa.
Onyesho la Tano; linamshuhudia Wakene akiwa nyumbani kwa Natala akimwambia juu ya suala la kumrithi akiwa kama mke wa marehemu kaka yake lakini Natala anapokataa Wakane anaamua kuchukua cheti cha shamba kwa nguvu. Natala anaamua kusimama kidete na kumzuia Wakene kitendo kilichopelekea wazozane Natala na Wakene. Mwisho katika onesho hili Tango aliyesadikika kuwa amefariki anarejea nyumbani na kukuta vurugu sebuleni kwake Natala na Wakene wakiwa wameshikana kuashiria kuna ugomvi. Wanapomuona wote wanaduwaa na kuishiwa nguvu, baadaye Natala anaamini kuwa Tango hakufa na anamsimulia mumewe yote yaliyokuwa yanamsibu pindi imesemekana amekufa na kuzikwa.
Mandhari; katika tamthiliya hii mandhari halisi imechorwa kama ifuatavyo; nyumbani- mahali ambapo walikuwa wakiishi Natala, Tango Mwina na watoto wao wawili ambao ni Bwanu na Alika; makaburini- ni mahali ambapo maziko ya mtu aliyezaniwa kuwa Tango yalifanyika; Gerezani- ni mahali alipofungwa Tango baada kukamatwa na polisi kwa kosa la uzururaji; mjini-hapa ndipo Tango alipokamatwa pamoja na watu wengine wakiwa wamelewa; mochwari (jengo la ufuo)-ndipo ilipokuwa imehifadhiwa maiti ya mtu aliyesadikika kuwa ni Tango Mwina.
Wahusika; mwandishi wa tamthiliya hii ameonesha wahusika ambao tumeweza kuwatenga katika makundi makuu matatu kutokana na uhusika wao kama inavyofafanuliwa hapa chini:
  • Mhusika mkuu; katika tamthiliya hii Natala ndiye mhusika mkuu kwani ndiye aliyebeba dhamira kuu ya ukombozi wa mwanamke kiutamaduni. Pia inatokana na ujasiri wake wa kuweza kupiga dhuluma yake na kupigana na wanaume waliotaka kuudhalilisha utu wake.
  • Wahusika wajenzi; hawa ni wahusika kama Kasisi-aliyeongoza mazishi kule makaburini; Chifu- huyu ni kiongozi anayependa rushwa hivyo anawakilisha viongozi wasiotenda haki kwa watu wao na hivyo anaibua dhamira kama rushwa na uongozi mbaya; mhudumu wa jengo la ufuo-amechorwa kama mtumishi asiyethamini utu wa mwanamke pale anapotaka kumbaka Natala.
  • Wahusika wasaidizi; mwandishi Kachora wahusika wanaomsaidia Natala katika kutimiza dhamira yake kuu baadhi yao ni Wakene- ambaye ni shemeji yake anayetaka kumdhulumu mali Natala baada ya kukataa kurithiwa; Mama Lime-aliyekuwa akimshawishi Natala akubali kuolewa na Wakene; Tango- amechorwa kama mume wa Natala na inaposemekana kuwa amefariki Natala anapangiwa kurithiwa na Wakene; Bwanu na Alika- ni watoto wa Natala na Tango Mwina. Wamemsaidia Natala kujenga dhamira ya malezi ya wototo; wahusika wengine wasaidizi ni pamoja na Bala, Mzee Balu na Tila ambaye ndiye mke halali wa Wakene.
Migogoro; Profesa Kithaka Wa Mberia katika tamthiliya hii ya “Natala” pia ameonesha migogoro amabayo tumeijadili katika makundi makuu mawili yani mgogoro wa nafsia na migogoro ya mtu na mtu au kikundi:
  • Mgogoro wa nafsi
Mgogoro huu unamkumba Natala baada ya kupata taarifa kuwa mumewe Tango amefariki na kuanza kuwaza/kufikiri jinsi atakavyoweza kuwalea watoto peke yake akawa analalamika moyoni akisema;
Dhiki gani hii? Kwanini ninyang’anywe mume? Msiba juu ya msiba! Majonzi juu ya majonzi…” (uk.9). Suluhisho la mgogoro huu ni Tango kurejea nyumbani na wote kujua Tango bado yu hai.
  • Mgogoro wa mtu na mtu
Natala na Wakene
Mgogoro huu ulitokana na Wakene kutaka kumrithi mke wa kaka yake ambaye ni Natala ili achukue mali zote pamoja na shamba. Natala anapokataa ndipo wanapoanza kunyang’nayana cheti cha shamba (uk.53-55) wanabishana wakisema;
Natala: kilete cheti!
Wakene: Nitakutwanga!
Natala: niguse uone! Tia mkono motoni.
Mama Lime: Wakene mtie adabu huyo mwanamke!”
suluhisho la mgogoro huu ni Tango kurejea nyumbani.
Natala na mhudumu wa jengo la ufuo (mochwari)
Mgogoro huu unatokea pale mhudumu anapomtaka kimapenzi Natala ili aweze kumpa maiti ya mume wake. Natala alipokataa akataka kumbaka na ndipo ugomvi ulipoanza na wawili hao kusukumana hali iliyopelekea mhudumu kuangushwa chini. Ukurasa wa (16-23) Natala akiigiza na Bala wanasema;
Natala: Haja yangu ni kuchukua maiti. Si kuona ofisi.
Bala: Kuona ofisi ni kuchukua maiti.
Natala: Yaani iko ofsini?”
Suluhisho la mgogoro huu ni zamu ya mhudumu yule kuisha na kuingia mhudumu mwingine aliyewapa maiti bila kuwadai chochote
Natala na Chifu
Mgogoro unatokana na kitendo cha Chifu kuzuia mazishi ya mwili wa mtu aliyesemekana kuwa Tango Mwina mumewe Natala akidai hawana kibari cha kuzika la sivyo watoe pesa (uk.30-35) chifu anasema;
Chifu: Mnafanya nini? Hamkumupata ujumbe wangu? Nilisema maiti isizikwe mpaka nifike… Mbona mnaidharau serikali namna hii?...
Natala: Tuliupata
Chifu: …kisha ikawaje?
Natala: Baada ya kukungoja kwa kitambo kirefu tulionelea tuendelee na mazishi.” Suluhisho la mgogoro huu lilipatikana baada ya mzee Palipali kuzungumza na chifu na kuahidi watamuona wakimaliza maziko.
Kwa ujumla Prof. Ken Walibora na Prof. Wa Mberia wameweza kuyatazama mambo kiyakinifu ikiwa na maana kuwa wanayazungumzia matatizo ya jamii za Afrika ya mashariki kama yalivyo bila kutumia mbinu ya kuficha. Wote kwa ujumla wameweza kuibua na kero zinazozikumba familia nyingi za kiafrika ikiwa ni sambamba na mila na tamaduni kandamizi kwa mwanamke mfano urithi wa mjane na mali zake.


MAREJELEO
Muhando, P na Balisidya, N. (1976). Fasihi na Sanaa za Maonesho. Dar es Salaam: T.P.H
Senkoro, F.E.M.K. (2011). Fasihi; Mfululizo wa lugha na Fasihi. Dar es Salaam: KAUTTU
Wamitila, K.W. (2003). Kamusi ya Fasihi; Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus publication limited.
Kitabu cha NATALA na kitabu cha SIKU NJEMA































Utata katika Fasili ya neno.


Fasili ya neno.
Katamba,(1994:38) anasema kuwa neno ni kipashio kidogo cha maana katika lugha ambacho kiana dhima kisarufi. Anaendelea kusema kuwa, neno linaweza kusimama pekee yake na kuleta maana bila kupachikwa vipande vingine.
Kwa mfano, neno childish (utoto) linaweza kutenganishwa na kubaki child (mtoto) na neno hili linatumika kiupwekeupweke kwa sababu ni neno linalojitegemea lakini hatuwezi kutenganisha kipande {-ish}kikasimaa pekee yake na kuleta maana.
TUKI, (2004: 305) katika kamusi ya Kiswahili sanifu wanadai kuwa neno ni mkusanyiko wa sauti zinazotamkwa au kuandikwa pamoja na kuleta maana.
Habwe & Karanja, (2007:71) wanafafanua kuwa neno ni kipashio cha kiisimu kinachoundwa na mofimu moja au zaidi. Wanaendelea kueleza kuwa dhana ya neno ni tata mno hasa katika kubainisha neno na vipashio vingine katika lugha. Kwa mzawa wa lugha yoyote ile, ni rahisi kutambua neno kutokana na vipashio vingine kwa kutumia ujuzi na mazoea ya matumizi ya lugha husika. Kwa mfano, miundo ifuatayo hutambuliwa na mzawa wa lugha ya Kiswahili kuwa ni maneno ya Kiswahili:
  1. Wanalima (ii) mwanfunzi (iii)shuleni (iii) kalamu
Hivyo basi, kutokana na maana hizo tunaweza kusema kuwa neno ni kipashio cha lugha kinachoundwa na mofu moja au zaidi ambayo inaweza kusimama pekee yake na kuleta maana katika lugha mahususi. Ingawa dhana hii ya neno imezua utata kutokana na watalaamu mbalimbali kuibuka na vigezo tofauti tofauti vya kufasili dhana hii na mipaka yake. Tukimchunguza Mdee, (2010:5) anadai kuwa kuna vigezo vikuu vitatu vya kufasili dhana hii ambavyo ni kipashio huru kisichogawanyika, maana ya neno kiothografia na maana ya neno kisarufi.
Hata hivyo, kwa mwanaisimu huwa ni vigumu kutoa kijelezi kamili cha dhana ya neno na badala yake fahiwa mbalimbali za dhana hii zimetumika kiutendaji. Baadh ya fahiwa zilizotumika kueleza dhana yaneno ni ,midhihiriko ya neno, muundo wa neno, neno kisarufi. Hapa tutajikita kuzungumzia fahiwa mbili za dhana ya neno yaani midhiriko ya neno na muundo wa neno kama ifuatavyo:


  1. Midhihiriko
Udhihirikaji ni utokeaji katika utendaji halisi wa kipashio cha kiisimu kilicho dhahiri. Dhana ya neno hujitokeza kiutendaji na midhihiriko kadhaa, udhihirikaji wa neno huweza kujitokeza kupitia dhana zifuatazo:
Udhihirikaji kileksimu; leksimu ni kipashio kidogo kabisa cha msamiati ambacho kina uwezo wa kusimama pekee yake kama kidahizo. Kwa upande mwingine kidahizo ni msamiati ambao huorodheshwa katika kamusi. Kwa kurejelea leksimu, midhihiriko ni miundo mbalimbali ya leksimu na huwa na maana ya kimsingi ingawa huenda ikatamkwa na kuendelezwa kwa njia tofauti (Habwe & Karanja, 2007:72). Kwa mfano kutokana na leksimu “lima” tunaweza kuwa na midhihiriko ifuatayo:
Lima----->lima, limiwa, alilima, hulima, mkulima, n.k
Matamshi tofauti na jinsi yanavyoandikwa; midhihiriko hii inarejelea maana sawa ya kimsingi ingawa inatamkwa na kuendelezwa kwa njia tofauti tofauti. Vile vile dhana ya midhihiriko katika neno kwa mujibu wa Saluhaya, (2010:79-80) anasema kuwa neno huweza kudhihirika kwa matamshi ambayo ni tofauti na linavyoandikwa. Pia Kihore na wenzake,(2003:43) anadai kuwa katika lugha ya Kiswahili kuna maumbo machache yasiyokuwa na uwiano wa kimatamshi na kimaandishi. Kwa mfano, maneno kama vile ng’e, mba, mbu, ngwe, nje na mbwa ni baadhi ya maneno ambayo huandikwa tofauti na jinsi yanavyoandikwa. Pia Saluhaya, (2010) anadai kuwa sababu zinazofanya maneno yatamkwe tofauti na jinsi yanvyoandikwa ni kama zifuatazo:
  1. Athari za usanifishaji uliofanywa na wazungu; kazi ya usanifishaji iliyofanywa na waingereza ambao asili ya lugha yao haihusiani na lugha ya Kiswahili. Wazungu ndio walioteua othografia ya Kiswahili chini ya mwingereza Profesa Fedrick Johnson ambaye ndiye aliyesimamia usanifishaji wa othografia ya Kiswahili akiwa kama katibu wa kamati ya usanifishaji wa lugha ya Kiswahili iliyoundwa mwaka 1930.
  2. Upungufu wa herufi za kuwakilisha sauti za lugha ya Kiswahili; lugha ya Kiswahili kama ilivyo kwa lugha nyingine nyingi haijitoshelezi katika herufi za kuwakilisha sauti zake. Hii ni kwa sababu lugha ya Kiswahili inatumia mfumo wa maandishi uliobuniwa kwa ajili ya lugha nyingine tofauti na lugha ya Kiswahili.
  3. Tatizo la kiothografia; tatizo hili husababishwa na baadhi ya maneno kuwakilishwa kimaandishi na herufi pungufu kuliko ilivyo katika matamshi yake. Kwa mfano maneno kama vile nchi, nje, nne, ni baadh ya maneno ambayo yana herufi pungufu.
  4. Athari za kimazingira; mara nyingi matamshi ya wasemaji wa lugha huweza kuathriwa na mazingira mbalimbali waliomo kiasi cha kuwafanya wasiweze kutamka maneno kama yalivyoandikwa.
Kwa hiyo, tukichunguza kwa kina dhana hii ya midhihiriko tunaweza kugundua kuwa midhihiriko katika neno hujitokeza kupitia utokeaji katika utendaji halisi wa kipashio cha kiisimu kilicho dhahiri. Vile vile neno huweza kudhuhirika kupitia matamshi ambayo ni tofauti na jinsi ambavyo huandikwa. Hivyo midhihiriko ya neno mara nyingi hujikita katika kuangalia maana za msingi za maneno husika.
  1. Muundo wa neno
Habwe & Karanja, (2007:73) wanafafanua kuwa njia nyingine ya kutambulisha neno ni kwa kurejelea miundo mabalimbali ya leksimu katika tungo kimaandishi au kiusemaji yaani kwa kuangalia muundo mahususi wa neno. Hivyo, kwa mfano katika kipengele cha midhihiriko, tumeweza kutoa mifano kama vile lima, limisha, mkulima, limiwa. Kwa upande wa muundo wa neno, maneno kama haya ni maneno manne tofauti licha ya kuwa yanarejelea maana moja sawa ya kimsingi. Miundo ya maneno katika lugha mbalimbali huwa kama ifuatavyo:
Muundo wa mofu tegemezi; katika muundo huu neno huwa limeundwa na sehemu kuu tatu ambazo ni viambishi awali, mzizi na viambishi tamati. Kila sehemu ya neno hilo huwa lina dhima yake kisarufi na kuwa sehemu kamili linalound neno hilo, ikitokea ukabadili sehemu mojawapo neno hupoteza maana ya msingi, kwa mfano,
  1. {Mwimbaji} mw-imb-a-ji
  2. {Anaimbisha} a-na-imb-ish-a
  3. {Watakapotuimbia} wa-ta-ka-po-tu-imb-i-a
Mofu kama hizi endapo zitasimama pekee yake haziwezi kuleta maana kamili bali hutegemea viambishi ili kukamilisha taarifa iliyokusudiwa.
Muundo wa mofu huru; katika muundo huu neno haliundwi na viambishi awali, mzizi na wala viambishi tamati bali kwalo huwa na mzizi au neno huru linajitosheleza kimaana pasipo kupachikwa viambishi. Mfano wa mofiu hizi ni pamoja na majina ya watu, majina ya mahali, majina ya miezi, majina ya nchi, na baadhi ya vielezi kwa mfano, Herman, Tanzania, Mwanza, Januari, polepole, wasiwasi, na maneno mengine yanayofanana na hayo.
Maneno kama hayo hapo juu ni mofu huru ambayo hayategemei viambishi vya aina yoyote na yanatoa taarifa kamili. Ikumbukwe kuwa maneno kama wasiwasi na polepole ni mofu huru kwani huwezi kuyagawa na yakabaki na maana ya msingi ile ile.
Muundo wa mofu ambatani; maneno haya huwa yanundwa na mizizi au mashina mawili tofauti tofauti yaliyounganishwa kwa pamoja kwa kuacha nafasi ama kutokuacha nafasi katika mizizi au mashina hayo ili kuwasilisha dhana moja kimaana. Aghalabu maneno haya huundwa kwa kuweka pamoja mizizi au mashina ya maneno mawili tofauti na kupelekea kibuka kwayo, mizizi au mashina hayo yaweza kuwa tegemezi au huru, kwa mfano, asikari kanzu, mwanajeshi, mwanahewa, bata mzinga, kipazasauti, kipimahewa, na maneno mengine kama hayo.
Kiukweli; maelezo kuhusu dhana ya neno ni tata, aghalabu huelezeka kutokana na vigezo mbalimbali vinavyotumika kufasili neno kuonekana ndicho kiini cha ugumu wa ufasili wa neno, pia tofauti za lugha huchangia kwa sababu lugha nazo hutofautikana kwa namna mbalimbali, wakati mwingine mizatamo tofauti tofauti huchangai pia kuifanya dhan hii kuwa ngumu, hivyo ni muhimu kwa wanafunzi wa kozi ya mofolojia kuelewa vigezo hivi kwa kuhusianisha mawazo ya watalaamu mbali mbali katika kujadili dhana hii ya neno. Kwa kuelewa dhana hii barabara itmwezesha mwana mofolojia kuweza kuyapanga maneno kutegemeana na vigezo vya uainishaji vilivyo elezwa hapo juu, ingawa kuna kigezo cha kisarufi hakija jadiliwa hapa kutokana na mawanda ya kazi yetu kuwa na kikomo cha vigezo vya midhihiriko na muuondo wa neno tu.


MAREJELEO
Habwe, J & Karanja, p.(2007). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili. Nairobi: Phoenix Publishers
Katamba, F. (1994). Morphology. London: Mac Millan Press Ltd
Kihore, Y.M, Massamba, D.P.B., Masanjila, Y.P. (2003). Sarufi Maumbo ya Kiswahili Sanifu
(SAMIKISA) Sekondari na Vyuo. Dar es salaam: TUKI.
Mdee, s. (2010). Nadahria na Historia ya Leksikografia. Dar es salaam: TUKI
Saluhaya, M.C. (2010). Kiswahili 1 Nadharia ya Lugha. Dar es salaam: STC Publishers.
TUKI, (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es salaam: Oxford University Press,
East Africa Ltd.

hakiki na tuma maoni au mapendekezo kuhusu makala hii ya andiko langu la uchunguandiko langu

ANDIKO LA UCHUNGU (Kwa shemeji zangu na wanangu)           NYAMBUYA OGUCHU,                            S.L.P 777666,       ...